Monday 24 December 2018

SINEMA ZA NGONO ZINAVYO ATHIRI VIJANA ULIMWENGUNI LEO-2


Tuendelee na mada ya wiki jana.
Zamani sinema za ngono zilikatazwa kabisa na serikali ya Mwalimu Nyerere  na hata awamu zilizofuata. Leo zinaonekana waziwazi katika simu na wanawake kwa wanaume wanazikodolea macho. Matokeo kuna kudhalilishana pande zote mbili. Hii ni kutokana na taswira za waigizaji wachache wenye maungo yasiyofikana na hali halisi za wanadamu wengi.
Starehe hii kama zilivyo nyingi za kisasa zimeletwa na utandawazi na teknolojia za Kizungu. Sisi Waafrika hatukuwa na matatizo ya ngono au ufanyaji mapenzi. Mwalimu Nyerere na viongozi waliopita wallifahamu hilo ndiyo maana wakalikataza.
Miaka 30 hadi 50 iliyopita hatukuwa na matatizo ya mapenzi.

Nilipohamia Uzunguni nilishangazwa jinsi wenzetu walivyo na matatizo makubwa ya ngono.
Hii ni kutokana na mosi hali ya hewa ya baridi, pili, biashara na uchumi wa kibepari unaouza kila kitu. Si kwamba Afrika hakukuwepo (au hakuna) uchumi huu, ila utamaduni wa mapenzi ulikuwa kawaida.  Tukiwa watoto tayari tunacheza ngoma na kutumia miili yetu bila kujali.
Sivyo Uzunguni.
 Watoto wadogo huanza kucheza kwa kuruka ruka badala ya kutikisa miili yao hasa sehemu za kati. Watu wazima hawana utamaduni huu, na watoto wa kiume hawapendi kabisa kucheza densi au kukatika viuno. Kwetu kukatika kiuno (chakacha, mathalan) , si hoja, kwa wenzetu ni matusi yanayopaswa kwenda kujifunza darasani. Ndiyo maana sinema za ngono ( au za matusi ) zikawa ( na zingali) jambo muhimu sana, Majuu.


Leo utamaduni huu umeenea si tu katika hizo sinema , pia, video na sanaa za maonesho ambapo wanawake maarufu huuza kazi zao, uchi,  au nusu uchi, kisanaa. Kwao ni jambo zito. Lakini mahusiano baina ya watu si huria kama inavyodhaniwa – na ndiyo maana sinema za ngono hutumiwa sana “kuchangamsha” hisia.
Tuchukue mfano wa tukio la wiki mbili zilizopita jiji la Bournemouth (tamka “Bonmuth") ....kusini mashariki ya Uingereza. Kijana wa miaka 20 alihukumiwa kifungo cha maisha na mahakama ya Winchester. Roy Thornton, alizoea kutazama sana sinema za ngono na kuvita bangi. Mseto huu ulikuwa Ibilis kwa mwanaume huyo aliyefanya kazi ya upishi.
 Mosi alipenda sinema za ubakaji (ngono ya nguvu) na pili, alipanga chumba na jirani mwanamke kijana (34) mzawa wa Venezuela, Marekani ya Kusini, Stela Domador- Kuzma. Haielezwi ilikuwaje.  Ila siku moja, ushetani wa bangi ulimpanda  kichwani, Roy Thornton akaingia chumbani kinguvu, akamchoma dada, Stela,  visu 17. Alipofariki sasa AKAINAJIS MAITI.

Hayo ndiyo matokeo ya hizi sinema, hususan zikichanganywa na dawa za kulevya. Na ndiyo mambo yanayoigwa sana Afrika karibuni.
Sasa sisi wenye ngoma motomoto, tunaoigwa na watu wengi duniani, tumejisahau na kuanza kuiga utumbo.  Matokeo vijana wetu wana shida tele za kimapenzi.  Wanawake wanalalamika wanaume hawana tena urijali. Wanaume wanalalamika wanawake hawajiheshimu, kila jambo uchi tu. Huu ni ugonjwa wa kisaikolojia uliostawi Uzunguni miongo mingi.
Leo Waafrika ni watu TUSIOJITAMBUA. Hatujui utajiri na uasilia wetu. Tunaiga mengi yanayotudhalilisha na kutuchuja.

Ilitoka, Mwananchi Jumapili, 16 Desemba, 2018


No comments:

Post a Comment