Saturday 30 November 2013

MASHUJAA WAWILI WA MFANO WALIOFARIKI MWEZI NOVEMBA…


Tarehe 23 Novemba 1963 wakati namalizia malizia darasa la pili,  tuliambiwa tusiende shule. Jana yake, Rais John F Kennedy wa Marekani alipigwa risasi akiwa ziarani mjini Texas. Nakumbuka Watanganyika (tulivyoitwa miaka hiyo ) tulivyosikitika. Rais Kennedy alipendwa sana. Marekani iliisaidia Tanganyika kwa  misaada na wataalamu wa kujitolea – walioitwa “Peace Corps.” Urafiki huu ulidhihirishwa na mifuko ya sembe na vyakula yenye picha ya mkono wa Mzungu na Mwafrika vimeshikana kirafiki.
Mwalimu Nyerere alipokaribishwa  na Rais John Kennedy na kuhutubia Ikulu ya Marekani- mwaka 1963. Walikuwa marafiki wakubwa. Miezi michache baadaye Rais Kennedy aliuawa.

Baada ya miaka mitano mdogo wake marehem, Robert F Kennedy naye aliuliwa kwa risasi wakati akifanya kampeni za Urais. Wengi walitazamia angekuwa kiongozi bora kama kaka mtu.
Toka walipouawa ndugu hawa, sinema mbalimbali na mandishi yametolewa kuhusu kisa na sababu. Aliyezungumziwa na anayeendelea kuongelewa ni marehem John Kennedy- rais aliyependwa kuzidi wote katika historia ya Marekani.