Friday 7 September 2018

... KUUHARIBU UHAI WETU KUPITIA MIMEA ILIYOBATILISHWA KWA GMO- Sehemu ya pili



Juma lililopita tulifahamishana kuhusu GMO.
Kabla ya kuendelea tukumbushane hulka ya biashara hususan huku nchi zilizoendelea. Siku hizi ni kawaida  kabisa kwa wateja, Uzunguni, kutaka kujua nini wananunua, nini kitakachoingia tumboni, tarehe gani  bidhaa itaoza au kukosa thamani, nk. Wasiojali sana ni maskini au wasiosoma. Lakini hata hawa hulazimika kuchunguza  pale maradhi yanapobisha hodi. Tutoe mfano...
Uzunguni kuna tatizo kubwa la “allergies”
Allergies ni  nini?


Haya ni maradhi ya kisasa,  ambayo nimedokezwa  yanashanyemelea Afrika kutokana na teknolojia inayokithiri pia. Huja pale kitu kinapoingia mwilini na kuushambulia kwa vile viungo vimeshindwa kukizuia mathalan vumbi, moshi au kiyoyozi. Dalili mahsusi ni kupiga sana  chafya- au kuvimba vipele unapokula au kujigusa na mmea fulani. Ndipo waganga husema : “Allergic reaction...”
Miaka michache iliyopita mteja wa Kizungu alikula chakula hoteli. Akafariki. Mwenye hoteli akashtakiwa kwa kutoeleza katika muhatasari wa vyakula kuwa kitoweo kilitumia mbegu (  karanga, korosho, nk). Marehemu alikuwa na hiyo “allergy” iliyosababishwa na kokwa (“nuts”)...
Hii mifano inadhihirisha namna ambavyo wafanya biashara hutakiwa  kuorodhesha Virutubishi, dawa   zilizotumika kuhifadhi (“preseravatives”) na  Uasilia ( Organic) wa bidhaa. Vile vile,  GMO.
Mbali na “allergy” -sasa hii GMO (“Genetically Modified Organism) – yaani vyakula vilivyobatilishwa-  vyatakiwa kuoneshwa, makasha ya bidhaa, kisheria.
Miaka kadhaa imekwisha toka nilipofurahi sana kufuma Unga wa Ugali unauzwa  London. Nilipoona “Made In Tanzania”- nikachangamka.  Kabla ya kulipia (kama ilivyo desturi) nikasoma mfuko. Unga ulitumia  GMO. ..
Kichwa upande sikuununua unga wa nyumbani.
Wapo  wasiojali wanakula nini. Wazungu wameshaona madhara na matatizo, sasa kwa kuwa sisi Afrika hatutahadhari sana, tunageuzwa soko la GMO
Mwaka 2004 , mtaalamu wa  mkusanyiko wa mashirika 170 ya maendeleo ya Ardhi Afrika (PELUM), Bw  Zakary Makanya- aliandika makala ndefu kushutumu  wanasayansi wa nchi zilizoendelea wanavyolitumia bara letu kama jaa la takataka- kusambaza  GMO. Alieleza sababu kumi na mbili kwanini Afrika isikubali GMO. Ni vizuri msomaji ukajaribu kumsoma mtandaoni. 
Alidai kilimo cha GMO ni kizuri kibiashara- huwafaidi wenye  mashamba makubwa. Ila kwa wakulima wadogo - unaa tu. Pili, akaonya mbolea au dawa zinazotumika kuzuia vijidudu zina madhara kwa ardhi na mimea. Ukitumia kilimo cha GMO inakubidi kununua dawa wanazouza wataalamu. Tegemeo hili la dawa ni sehemu ya biashara. Akasisitiza Waafrika tumetumia mbegu asilia kwa karne nyingi. Hatuhitaji dawa haribifu. Kwa mfano sasa hivi kuna kampuni (iliyoshajenga makao yake Dar es Salaam) - Mosanto - kazi yake ni kuendeleza kilimo hiki. Swali ni je viongozi wetu wanaelewa vipi madhara na faida za GMO? Je utafiti gani umefanywa na Waafrika tusijeharibiwa? Hadi sasa Zambia, Sudan, Angola na Benin zimeikataa  GMO – ilhali Ethiopia, Burkina Faso na Afrika Kusini zimechangamkia sayansi hii. Tajiri mkubwa duniani Bill Gates amepingwa sana karibuni kwa kusisitiza anasaidia kilimo Afrika kupitia GMO.
Wakati mijadala ikiendelea, kila msomaji anatakiwa kuchimba zaidi kuhusu mada hii. Hatari zake kama tulivyotaja sigara wiki jana hazijaeleweka. Tufungue macho.

-ilichapwa Mwananchi Jumapili, 17 Juni, 2018.



           




No comments:

Post a Comment