Wednesday 12 October 2016

VIPI TATIZO LA FIGO LAZIDI KUATHIRI AFYA ZA WAAFRIKA? - Sehemu 1



Tiba na afya za dunia yetu zimegawanyika sehemu mbili kuu.
 Magharibi ni uganga wa Kizungu unaotumia sayansi iliyofikia kilele karne ya 19 na 20. Moja ya nguzo zake kuu ni kutibu kwa kunyamazisha- kupitia sindano, dawa na upasuaji. Tiba ya Kizungu ndiyo inayotawala dunia yetu na ndiyo mara nyingi Wabongo wanaojiweza wakiugua siku hizi husafrishwa nje  kutibiwa.
Tiba za mashariki zinaongozwa na ustaarabu wa Kihindi na Kichina. Wahindi hutumia mwenendo uitwao Ayurveda. Tiba hii yenye zaidi ya miaka elfu mbili huangalia mwili mzima ukoje kabla ya kuushughulikia. Wachina wanao pia mtindo huo huo, unaotazama mtiririko wa nguvu mwilini badala ya dosari. Utaratibu wa Kichina na Kihindi kijumla hautibu tatizo moja kama  Wakizungu. Kwa wazungu mathalani ukiumwa kichwa utapewa dawa ya kuyaondoa maumivu hayo.

 Kwa Ayuverda na mtindo wa Wachina huchunguza mahusiano ya mwili mzima yakoje badala ya kitu kimoja. Wachina hugawa mwili kufuatana na sheria tano kuu zinazofuata maumbile yaani mti (mbao), maji, chuma, moto, ardhi au dunia.  Utaratibu huu hutumia tiba ya sindano (Accupuncture) ambazo husisimua umeme mwilini. Wahindi na Wachina wanaamini miili yetu ni sehemu ya sayari za dunia na ina mitiririko ya umeme isiyohitaji sana dawa za nje kuugangua mwili.
Tofauti ya matibabu na namna ya kutibu kati ya Magharibi na Mashariki haikuwepo zamani. Wazungu  walioanisha unajimu, utabiri, dawa asilia na mazingira (maumbile) kukagua na kugangua. Utaratibu huo ulifutwa kutokana na kukua mfumo wa kibepari na dini (Ukristo) vilivyotaka tiba za haraka na kugeuza uganga kuwa wa mashindano na malipo.
Je tofauti hii huonekanaje?
Ukiingia hospitali yeyote ya kisasa  (Kizungu) mganga anapokuona hujali zaidi kuondoa haraka adha inayokukabili. Mfano mzuri ni huko kuumwa na kichwa. Atajaribu kutafuta ufumbuzi wa kuondoa maumivu, hususan kwa vidonge.
Linganisha na tiba za Ayuverda au Kichina ambapo uchunguzi huangalia je unalalaje? Ndoto zako zikoje? Badala ya kupima mapafu ataangalia ncha ya ulimi. Je ulimi mwekundu nchani? Kama ulimi mwekundu atakuuliza je vipi unajisikiaje? Una hamaki za ghafla ghafla? Mbali na  hayo tiba hii itaangalia harufu ya mwili wako, ngozi, nk.
Tiba zote mbili hukagua pia mapigo ya moyo kutaka kujua mtiririko wa damu ukoje. Ila tofauti iko katika tiba, Mara nyingi unapokwenda kwa Mchina atakupa dawa ya kutibu mtiririko wa nguvu na umeme mwilini.
Tiba hizi zenye mitazamo miwili tofauti zimeanza  kuoanishwa nchi zinazoendelea. Wapo waganga wa Kizungu walio tayari kukubali baadhi ya tiba za Mashariki, mathalan Accupucture (tiba ya sindano), lakini si wote. Baadhi ya hospitali za Ulaya zimefungua idara zinazokubali tiba hizi za sindano na pia kuafiki usingaji kwa wagonjwa  wa saratani na maradhi mengine makali.
Kati ya tatizo kubwa la tiba za Kizungu ni madhara ya dawa kali zinazotumika kutibu maradhi makubwa makubwa. Madhara haya (yanayoitwa “side effects” kitaaluma), yameanza kuongezeka kutokana na dawa za maabara zisizojali sana hatima ya mwili. Hii ni kutokana na lengo la tiba za Magharibi ambazo ni kuondoa tu tatizo moja kuu kinyume cha athari- jumla. Uganga wa mashariki humwangalia mtu mzima badala ya kipengele tu cha maradhi yake. Tuchukue mfano wa shinikizo la moyo au presha.  Kambi  nzima ya uponyaji ulimwenguni inakubali kuwa maradhi ya moyo husababishwa na mambo makuu manne : unene au kitambi, maisha ya haraka haraka na tafrani, mshtuko wa ghafla ,  mirathi au kurithi kifamilia.
Kinachotofautiana ni tiba.
Mara nyingi Uzunguni hutoa dawa za kupunguza shinikizo hilo.
Kwa watu wa mashariki pamoja na tiba mbalimbali za dawa za miti na mimea au Accupunture, huhimiza usingaji, mapumziko na hata kufanya shughuli zinazotulizana moyo ( na roho); kupiga muziki, kuchora , kufanya kazi za bustani ...pole pole Wazungu wameanza kupokea fikra hizi.
Yamkini dunia ya leo inaanza kuoanisha tiba hizi mbili zinazokinzana lakini ambazo zamani zilikaribiana.
Kwetu Afrika pia tunazo tiba mbalimbali.
Tiba zetu zimegawanyika sehemu mbili: mazingaumbwe au uchawi;  na miti shamba au mimea na mali asili. Ingawa kuna utajiri mkubwa wa kuganga na kugangua bado serikali zetu hazijatambua umuhimu wa tiba asilia. Bado tasnia hii ni ndogo na tunategemea sana dawa na matibabu ya Kizungu. Egemeo hili kwa Wazungu limezidi kiasi ambacho maradhi makubwa makubwa yanatuua haraka sana.
Mbali na tiba hizo bado sisi si wepesi kukinga. Kinga maradhi inategemea sana kufahamu mwili ukoje na nini tunapaswa kufanya kuudhibiti.
 Kati ya mambo tunayopaswa kufahamu ni viungo vyetu. Wachina wanaamini kuwa tumbo ni kiungo muhimu kuliko vyote. Fikra hii inatokana na kwamba kila siku tunakula milo mitatu na vitu vingine vidogo vidogo. Kuweka huku vitu mwilini hutegemea sana tumbo, ini, uwengo, figo na moyo kufanya kazi zake. Karibuni, figo,  imekuwa tatizo la Waafrika.  Kitakwimu, zamani figo ilikuwa tatizo la wazee lakini leo watu wenye umri wa miaka thelathini hadi arobaini wana tatizo la figo. Figo kazi yake ni kuchuja umaji maji mwilini.
Kwa kuwa siku hizi hatupiki vyakula asilia, kutokana na maisha ya kukimbia kutafuta riziki, fedha na kazi, tunakula vyakula visivyotengenezwa vizuri. Vyakula vyetu vina  ladha ya kuvutia lakini vinaharibu figo. Kwanini figo? Kwa vile figo kazi yake ni kuchuja maji na masalia yake. Wiki hii mtandao umesambaza ilani kuwaasa wazungumzaji wa Kiswahili  kujali zaidi figo. Kati ya tahadhari zilizotolewa ni kunywa maji ya uvuguvugu (Wachina na Marasta husisitiza maji moto) badala ya baridi, kutokula vyakula vyenye chumvi na pilipili nyingi , sukari (Watanzania tunapenda sana Soda na Cocacola au chai yenye sukari nyingi), kutokunwya maji na kula chakula usiku sana. Nadhari inazingatia kuwa kadri unavyokula sana usiku au kuweka ladha nyingi katika mlo wako ndivyo unavyozipa figo zako mbili kazi na mizigo mizito. Unapokula usiku sharti uhakikishe unakaa saa tatu kabla ya kulala. Matunzo ya figo yako ni dhamana ya afya shauri bila chujio hilo uchafu huathiri viungo mbalimbali mwilini mathalan kibofu, ngozi, damu nk.


-Ilichapishwa 



No comments:

Post a Comment