Wednesday 12 October 2016

VIPI TATIZO LA FIGO LAZIDI KUATHIRI AFYA ZA WAAFRIKA?- Sehemu ya 2




Majuma matatu yaliyopita safu hii ilizungumzia  tatizo la maradhi ya figo. Punde tu wasomaji kadhaa waliniandikia kuulizia habari zaidi.
Takwimu za afya Ulaya zinasema figo huandama zaidi watu weusi.
Ingawa bara lina kila aina ya virutubisho , mazao na hali ya hewa safi, bado hatujijali kiafya.
Je maradhi ya figo yanaepukika? Na kuanzia, figo ziko wapi na kazi yake ni nini?
Figo mbili ziko , juu ya nyonga,  chini ya ubavu, mgongoni. Kawaida mabondia wanapodundana, wakikaribiana, kila mmoja hujaribu kupiga figo. Kwanini figo idundwe?

Figo na kibofu cha mkojo ni wachujaji maji machafu  mwilini. Wachina huziiita figo hakimu mkuu. Bila figo ni jangwa.  Baada ya kula na kunywa lazima amri itolewe kupeleka umaji maji na damu inayotakiwa mwilini kutokana na vyakula na vinywaji. Visivyotakiwa hutimuliwa.  Wanasayansi wanatueleza  asilimia 75  ya mwili ni maji  katika musuli na minofu. Kiasi hutofautiana kati wanawake na wanaume.
Kazi ya kusafisha na kupiga deki hufikia kilele saa tisa hadi  moja jioni, kila siku. Ndiyo maana wengi husikia uchovu au kutokuwa na nguvu saa hizo. Kazi kuu ya kutenga hufanywa pia saa tisa za usiku hadi kumi na moja alfajiri.
Sasa kwanini matatizo ya figo yamezidi sana miaka hii kwetu weusi ?
Kwanza  tuzingatie kuwa wanadamu hatufuati tena kanuni kiasilia. Zamani tulikuwa kama wanyama. Saa ya kulala ni kila kiza kikiingia na kuamka mwangaza unapochungulia. Hilo “likafutwa” na badala yake siku hizi tuna washa taa ili tuendelee kuangalia sinema na kukesha.Ubundi...
Halafu ulaji.
Wazungu wana desturi ya  kula mapema. Ukanda wa nchi za Scandinavia mathalan hula chakula cha mwisho saa kumi na moja na kumbi mbili za jioni. Ikishapita saa mbili za usiku, wenzetu hawali misosi mizito. Husema si vizuri kwenda kitandani na tumbo lililojaa.
Ukitazama Waafrika wengi, hasa tunaioishi mijini siku hizi, tuna tabia ya kula usiku sana. Hii ni kutokana na mbio za maisha na” kutokuwa na muda.” Unatoka kazini hadi umalize shughul, upike , ule ni saa nne za usiku. Mara baada ya kula usingizi huo tunajirusha vitandani.
Tatizo kubwa sana.
Mwanadamu unatakiwa ukae saa tatu nzima kabla ya kulala, baada ya kula. Sababu kuu ni umeng’enywaji wa chakula. Ukila kisha ukaendelea na shughuli ndogo ndogo hadi saa tatu zikipita halafu ndiyo ulale, unakuwa umeupa mwili muda wa kufanya kazi yake, kiufanisi.
 Pili, wakati tumelala, tumbo huwa kazini. Sasa kama tumbo limejaa  (kama umekula nne au tano), ukiwa umelala, viungo havipumziki.
Juu ya hilo sasa, huku umeng’enywaji ukiendelea, hakimu au mchujaji wa chakula kilicholiwa jana yake, kuondoa kinyesi na mikojo, ni figo na kibofu.  Haya yasipofanywa kwa wakati wake huwa kazi ya ziada kwa viungo hivyo.
Ni kama mtu kupewa kazi moja ya kufanya halafu ukaongezewa nyingine kabla ya kuimaliza. Hakuna ufanifu, ufanisi, au uendelezwaji...
Tatizo la pili ni aina ya vyakula.
Zamani tulikula vyakula asilia. Mapishi yalizingatia uasilia wake. Leo kutokana na “mbio za mapanya” wengi hatupiki. Tukiwa  mitaani, tunakimbilia “chips” kwa nyama. Mafuta yanayopikia mitaani huwa yameshatumika muda mrefu. NI kama sumu mwilini. Ongezea sasa chumvi na ghasia nyingine za ladha. Suala la” ladha” ni janga kubwa sana kwetu watu weusi. Sisi  ( na wenzetu wa Marekani ya Kusini , Karibi, na Asia) tunapenda sana chumvi, pilipili, nk. Tunathamini  ladha badala ya virutubisho vya misosi. Mbali na chumvi, lazima tubwie vitu vingine wakati tunakula. Kunywa huku unakula ni kazi kubwa kwa tumbo na figo. Wengi hukata kiu wakila kwa chai, Cocacola, bia au soda. Hapa kuna mawili. Chumvi na sukari pamoja ni unaa. Vikifika mwilini lazima vichambuliwe. Hiyo si kazi tu ya tumbo (hydrocholoric acid kwa waliosomea kimia mashuleni), uwengu, na ini. Ni mtihani kwa hakimu au mchujaji wa maji maji mwilini yaani figo. Ukitaka kunywa chochote, kinywe saa moja au zaidi kabla au baada ya msosi. Si kunywa na chakula. Na ni bora maji kuliko sukari sukari.
Sasa hapa tunamzungumzia mtu mwenye afya na mwili wa kawaida. Ukiwa mnene au usiyefanya mazoezi ndiyo kabisa unajichongea. Ndiyo maana tatizo la kibofu, figo, presha nk huwa kali zaidi kwa wanene au wana vitambi. Hata hivyo haina maana kwamba usipokuwa mnene, weka sana chumvi nyingi katika chakula chako.  
Je matatizo ya figo huwaje?
Dalili ziko nyingi.
Uchovu usioeleweka, miguu na mikono kuvimba, pumzi za shida, kujisikia ovyo ovyo (kichefu chefu) bila sababu maalum- mathalan kama si mja mzito au uliyekunywa sana pombe jana. Kutapika tapika bila sababu.  Pili, mkojo. Kuwa na damu katika mkojo. Kutokojoa sawa sawa au kukojoa kojoa mara kwa mara. Kuwa na maumivu ukifanya haja ndogo. Haja hiyo ndogo kuwa na harufu au rangi isiyo ya kawaida, kijani, kahawia au  mapovu mapovu, utadhani unarusha sabuni ya Omo.
 Jingine ni maumivu. Maumivu  sehemu za siri hasa korodani kwa wanaume. Maumivu kinenani au tumboni. Maumivu nyongani, chini ya mbavu , nyuma, zilipo figo zenyewe. Kwa watoto huwa hawana nguvu , hukereka ovyo au wana mkojo wenye harufu mbaya sana.
Kupima ni vyema kwenda kwa mganga kuangaliwa mkojo na damu. Kati ya tiba asilia ni magadi na kula vyakula vyenye virutubisho. Mathalan vitunguu, vitunguu saumu,matunda hasa yale yenye mbegu mbegu ndogo ndani (Berries), matufaha,kabichi, koliflawa, samaki na kutumia mafuta ya mzaituni kupikia au kwenye Salad.
Salad na Mwafrika. Mmh.
 Ni muhimu sana kula Salad na chakula. Salad hii iwe ya mboga mbichi za majani : nyanya, tango, nazi, parachichi, mbegu mbegu mbichi (korosho, ulozi, karanga) nk. Watu weusi tuna tabia ya kuweka chumvi hadi katika Salad yaani mboga za majani. Tumezidi. Hili linachangia sana kuumiza figo.
Juu ya yote haya tunapofanya mazoezi ya viungo na kulala muda unaotakiwa wa saa 7-8 kwa siku, tunazipunguzia figo, mzigo.


No comments:

Post a Comment