Showing posts with label Familia na Jamii. Show all posts
Showing posts with label Familia na Jamii. Show all posts

Tuesday, 10 September 2013

MTINDO WA KISASA WA NYWELE UNAHARIBU AFYA ZA WANAWAKE WEUSI


Watu wa kabila la Chwi kule Ghana wanaozungumza lugha iitwayo Tshi wana methali kuhusu umuhimu wa kupendeza. Inashauri: “Ikiwa mwenda wazimu ataiba nguo zako na kukimbia nazo wakati wewe uko majini unaoga, itakuwa vyema utafute angalau kipande cha kitambaa ujifunge  wakati unamkimbiza maana usipofanya vile watazamaji watadhani na wewe umeheuka.”
Hakuna mwanaume ambaye hajawahi kupayukiwa kuwa asuburi wakati ndugu yake wa kike anajipodoa akijiremba. Na kati ya mapambo yote nywele zinaongoza foleni. Mwanaume waweza kutoka bila kuchana nywele, unaweza ukawa nusu kipara (kama mimi mwandishi) lakini hujali mradi u msafi utatoka zako mitaani. Kwa mwanamke kujisanifu nywele ni tendo muhimu sana. Ndiyo maana waandishi mbalimbali wa hadithi hawakosi maelezo ya ususi ndani ya riwaya zao.


Monday, 17 June 2013

WATOTO WETU WANAVYOANZA KUATHIRIKA NA HALI YA KISIASA NCHINI


Wakati n’naishi Brazili miaka 20 iliyopita moja ya woga mkubwa ulioenea ni hatari ya watoto wadogo mijini. Hatari gani?
Sikiliza ...
Siku moja Jumapili  n’natembea ufukwe maarufu wa Copacabana  jijini Rio De Janeiro. Hapa pana eneo kubwa sana la kuogelea, wanawake warembo, majumba ya starehe, migahawa, magari, minazi na starehe za kuotea tu paukwa pakawa. Jaribu kulinganisha ufukwe huu na Coco Beach , Dar es Salaam. Anzia pale kilima kinachoelekea barabara ya Chake Chake ongoza hadi Kivukoni penye wauza samaki na boti linalovusha watu. Sema badala ya hospitali ya Ocean Road na Ikulu sasa weka majumba hayo niliyozungumzia ya starehe na sehemu ndefu  sana maridadi za kufanya mazoezi na kuogelea.
Watalii walipahusudu. Na hii si yote- ufukwe  wa Copacabana umeunganika na  Ipanema na Leblon, bichi nyingine mashuhuri za jiji. Wabrazili husema Mwenyezi Mungu aliuumba ulimwengu mzima kwa siku sita, ile ya saba akakaa kitako akikamilisha Rio De Janeiro peke yake. Nilikua na tabia ya kwenda kuogelea  na kufanya mazoezi pale mara mbili tatu kwa juma.