Wakati n’naishi Brazili miaka 20 iliyopita moja ya woga
mkubwa ulioenea ni hatari ya watoto wadogo mijini. Hatari gani?
Sikiliza ...
Siku moja Jumapili n’natembea ufukwe maarufu wa Copacabana jijini Rio De Janeiro. Hapa pana eneo kubwa
sana la kuogelea, wanawake warembo, majumba ya starehe, migahawa, magari,
minazi na starehe za kuotea tu paukwa pakawa. Jaribu kulinganisha ufukwe huu na
Coco Beach , Dar es Salaam. Anzia pale kilima kinachoelekea barabara ya Chake
Chake ongoza hadi Kivukoni penye wauza samaki na boti linalovusha watu. Sema
badala ya hospitali ya Ocean Road na Ikulu sasa weka majumba hayo
niliyozungumzia ya starehe na sehemu ndefu sana maridadi za kufanya mazoezi na kuogelea.
Watalii walipahusudu. Na hii si yote- ufukwe wa Copacabana umeunganika na Ipanema na Leblon, bichi nyingine mashuhuri za
jiji. Wabrazili husema Mwenyezi Mungu aliuumba ulimwengu mzima kwa siku sita,
ile ya saba akakaa kitako akikamilisha Rio De Janeiro peke yake. Nilikua na
tabia ya kwenda kuogelea na kufanya
mazoezi pale mara mbili tatu kwa juma.