Sunday 21 April 2013

TATIZO KUBWA LA VIRUSI SUGU LEO LIMETOKANA NA UTOAJI DAWA KALI KIHOLELA...


Enzi hizo hatukua na UKIMWI.
Magonjwa ya zinaa hayakuua mtu. Dalili yake ilikuwa kuwashwa na kujisikia vibaya wakati wa kwenda haja ndogo tu, basi.  Yakikuzidia  unazunguka zunguka mitaani unanunua dawa  rangi ya chungwa na manjano- kidonge cha “tetracylene”- aghali ndiyo; lakini kinamaliza kabisa tatizo.
Baadaye miaka ya Themanini UKIMWI ukatangaza ufalme.
UKIMWI haukuponywa kwa kidonge kama hicho.

 Na hata baada ya miaka thelathini, UKIMWI uliposhaanza kutibika- ( nchi zilizoendelea), haikua kidonge kimoja. Vingi.  Tena bei yake si ya porojo. Sijasikia mtu anayeweza kuingia tu sehemu akanunua msururu wa vidonge vya kutibu UKIMWI. Tiba hii ilihimili lakini haijaondoa kirusi, abadan.


 Kawaida kirusi cha UKIMWI huwa kinamshinda mwanadamu kwa vile hushambulia mfumo mzima wa “kinga maradhi” mwilini.  Ingekua kirusi hiki hushambulia tu ingetosha kuzuilika kama ambavyo virusi vingine huzuilika-  kule kubadilika badilika kwake ndiyo kiini cha  zogo. Ndiyo maana Waswahili (tulivyo wabunifu) tukaukatia ugonjwa majina kama “ngoma”, “bomu”  “mdudu,” nk.
Watafiti lakini hawajalala.  Karibuni wametangaza kuanza kuelewa namna kirusi cha UKIMWI kinavyotekeleza ufisi wake. Waganga hao Dk Barton Haynes na John Mascola  walifanya majaribio kwa mgonjwa wa UKIMWI toka Afrika na kuchora ramani (“mapping”) ya mwenendo mzima. Hatimaye, tiba iko karibu ndivyo jarida la VR-Zone.Com  la Marekani lilivyotangaza kwa hamasa juma lililopita.
Hoja niliyoieleza hapa inaonyesha namna matangazo ya tiba za magonjwa mbalimbali zinazowasakama wanadamu yalivyo muhimu.
Vijana wa shule ya sekondari ya Mwandege, mkoa wa Pwani mwaka 2009. Taifa la kesho. Baadhi yao watakuja kuwa wataalamu wetu. Picha na F Macha

Mbali na  UKIMWI yapo maradhi yenye virusi vikali (yanayoendelea kutusakama wanadamu) mathalan- Malaria, Saratani na Kifua Kikuu kilichoanza kurejea karibuni...
Tatizo haliko katika haya maradhi bali katika “sugu” ambayo virusi vimejenga. Sikilizeni kisa kifupi.
Takriban miaka 15 iliyopita nilipohamia hapa Uingereza niliwahi kwenda zahanati ndogo ya kitongoji ninachoishi shauri ya mafua makali. Kawaida mafua ni ugonjwa katili sana jamii hizi za nchi baridi – huja majira yanapobadilika  mwezi Mei ( toka msimu wa baridi kuingia joto) na Novemba ( joto kuisha na kipupwe kuanza). Kufika kwa mganga akanipima presha, moyo, pumzi nk akasema niko sawa kabisa.
“Lakini daktari silali, usiku kucha napiga chafya.”
Akaniangalia kwa macho yenye mseto wa  huruma na cheko.
“Sikiliza. Wewe mzima kabisa bwa’ mkubwa; moyo na mwili wako viko shwari  shauri unafanya mazoezi, unajiangalia; huvuti sigara, unajali unachokula, afya yako kama ya kijana wa miaka 20 (nilikua na miaka arobaini). Nenda zako tu nyumbani kapumzike. Usitoke toke; kunywa maji kwa wingi, lala kwa muda mrefu. Utapona tu.”
Duu, nikamwona mganga yule (ambaye aliwahi pia kufanya kazi Tanzania) kama ana mipango mibaya nami.
“Naomba unipe dawa kali daktari. Siwezi nikakaa nyumbani na mafua, bila dawa yeyote. Unajua mafua yanaua hapa kwenu Ulaya?”
Akacheka.
“Nimeifanya kazi hii karibu miaka 30. Usipende sana kunywa kunywa dawa. Nenda zako tu nyumbani kapumzike. Baada ya siku tatu ukiona hali mbaya rudi tena nitakupa hiyo dawa kali unayoitaka.”
Roho iliudhika sana. Nikaenda zangu nyumbani kichwa upande. Usiku nilitokwa jasho, koo liliniwasha, (tunaweza kufananisha mafua ya Kizungu na Malaria) nikalala tu.  Kama alivyoshauri nikawa nakunywa  maji kwa wingi. Na kweli baada ya siku tatu ahueni, hiyo. Siku tano  kujiri, nikapona.
Sasa fundisho nini?
Waganga wa Kizungu siku hizi hawatoi kiua vijasumu -  Kiingereza “anti-biotics” -kama ile niliyoongelea mwanzoni, yaani Tetracyclene, ovyo.  Kuna wimbi lililozuka na kuenea kwamba kutumia sana dawa kali kutibu kila aina ya maradhi yanayotukabili kumejenga “sugu” kati ya mamia ya virusi pilipili vinavyotushambulia.
Mwezi uliopita Mganga Mkuu wa Uingereza Profesa Sally Davies  alihojiwa na runinga ya SKY akasema virusi vingi vimekua sugu hivyo tuna hatari ya kukosa tiba ya maradhi na kurejea hali mbaya na ya kizamani  karne ya 19.  Mganga mkuu huyu aliyehitimu  mwaka 1972 alilinganisha  hatari hii na ugaidi wa kidini unaoukabili ulimwengu wetu sasa hivi.
Tatizo la msingi akadai, ni biashara. Makampuni makubwa makubwa yanayowekezea utafiti wa dawa za kukinga maradhi (kama UKIMWI mathalan) “hayatengenezi fedha” kuvumbua dawa mpya. Toka mwaka 1987  hapajagunduliwa hata dawa moja mpya. Makampuni makubwa yanaona bora tu kuuza dawa zile zile kwa wateja wanaoendelea kuugua na hatimaye kufa maana haiathiri biashara.
 “Unapoweka dawa mpya katika madawati ya maduka wahitaji kwanza wateja wachukue muda kuzizoea; si rahisi kuuza.” Alidai.
Katika miaka mitano iliyopita virusi vikali kama E-Coli (anayekaa katika nyama mbichi kutokea  kinyesi mithili  michango na tegu)  vimekua kwa asilimia 60  ilhali kifua kikuu kimerejea kwa kasi. Miaka sitini iliyopita kifua kikuu kilikua na ushetani huo huo wa UKIMWI ulivyo leo.
Wiki jana niliongea na mganga mstaafu ( wa kigeni) Tanzania -hakupenda kutangazwa jina. Alisema leo asilimia 80 ya watoto kwetu wanapewa dawa kali kwa maradhi madogo madogo. “Kinachotakiwa ni kama asilimia 20 tu; asilimia 80 ni nyingi sana.”
Akasema sisi Wabongo tumeshazoea kwamba kila ugonjwa lazima uandikiwe kiua sumu (anti-biotics)- zahanatini. Utoaji huu wa dawa ni mbinu  tu kutajirisha  wafanyabiashara wanaouza dawa na hujenga sugu ya maradhi.
Utafiti uliofanywa mwaka 2010 hadi 2011 na waganga hospitali ya KCMC , Moshi wakiongozwa na  Judith Gwimile ulithibitisha watoto wadogo wamekua wakipewa viua sumu  kwa magonjwa  ya kuhara na kukohoa. Utafiti huo uliochapishwa  jarida la “Pan African Medical Journal” Agosti mwaka jana, unathibitisha dhana iliyopitwa na wakati. Kutoa dawa hizi kali kwa maradhi yasiyo na virusi vikali sana hujenga  mazoea na “sugu” katika miili ya wahusika kiasi ambacho wakiugua baadaye si rahisi kupona. Tabia hii imepingwa na kutajwa pia na shirika la Afya duniani WHO na wataalamu mbalimbali nchi zilizoendelea. Lengo lake ni kutengeneza tu fedha juu ya migongo ya walala hoi wanaohadaiwa kuwa kila ugonjwa unahitaji dawa kali.
Mwandishi wa mambo ya maradhi, Doug Kaufmann kaandika karibuni mtandaoni kuwa viua sumu huteketeza  vile virusi  rafiki vinavyopambana na virusi vibaya tumboni. “Nafasi yake huchukuliwa na kuvu au uyoga anayedhoofisha kinga maradhi na waweza  kusababisha  saratani.” 



  Ilitoka pia Mwananchi Jumapili....



No comments:

Post a Comment