Thursday 13 December 2012

NINI MSINGI WA TATIZO LA WAISLAMU WANAOHARIBU MAKANISA NA AMANI AFRIKA? -Sehem ya 1


Sijui wasomaji wangapi tunamkumbuka mwanamuziki mashuhuri wa Nigeria, Fela Anikulapo Kuti aliyefariki 1997 akiwa na umri wa miaka 59?  Fela alikuwa binam wa mwandishi maarufu, Wole Soyinka (pichani) aliyeshinda tuzo la fasihi (Nobel) duniani 1986.

Pamoja na kipaji cha muziki (utunzi wenye ujumbe mzito, kuimba, kupiga saxafoni, ngoma na piano) Fela hakua mwoga.  Alikuwa mmoja wa wanamuziki wachache Afrika ambaye hakusita si tu kuimba ukweli, bali tayari kupambana na serikali ya nchi yake na kukemea ufisadi na rushwa vilivyoinyea(na bado vinaendelea) Nigeria.

Serikali na majeshi yalimchukia na kumwandama kiasi ambacho mwaka 1977 askari elfu moja walivamia makao makuu ya bendi yake -Afrika 70-  wakampiga yeye, wake zake na wanabendi halafu  wakaharibu kila kitu. Ndani ya vurugu hiyo walimtupa mamake Fela (Funmilayo) dirishani – baadaye akafia hospitalini. Fela aliudhika sana akatunga  nyimbo mbili kuishutumu serikali na askari wadhalimu (“Coffin for Head of State” na “Unknown Soldier”) na kulipeleka jeneza la mama mzazi makao makuu ya jeshi yaliyoongozwa na Jenerali Olusegun Obasanjo(aliyekuja kuwa Rais). Licha ya kipigo,  baadaye alitafutiwa vijisababu akafungwa jela miaka mitano kwa msimamo usiokua na woga wala unafiki.
Tuangalie dhana ya unafiki.
Fela Kuti alioa wake 27 (aliowaita malkia ), mwaka 1977;  waliimba na kucheza naye jukwaani.  
<--more--!>

Akijitetea katika moja ya mahojiano yake Majuu alisema.
“Utamkuta mtu kaoa. Wakati mkewe yuko usingizini atatoka nje na kulala na wengine. Ni bora akiwaleta hawa wanawake wote nyumbani badala ya kuhangaika ovyo mitaani.”
Kitabu cha maisha yake kilichoandikwa na Carlos Moore (“Fela- this bitch of a life”, 1982) kinawahoji  wake zake 15 wanaofafanua kwanini walimhusudu.  Omolora Shosanya, mathalan, anakiri alimpenda Fela  kwa akili, ujasiri,  mtazamo wake na  kuwa mpenzi mzuri.
Jambo la pili lahusu mila.
Nigeria na mikoa yake...

 Nigeria inayo makabila mengi lakini matatu muhimu ni Waigbo, Wahausa na Wayoruba. Fela alihimiza sana misingi ya Wayoruba (kabila lake) kwa  kuvaa, kuimba, kupamba jukwaa, kucheza na kutambika mara kwa mara. Alisisitiza hilo kwa kubadili jina la Fela Ransom Kuti kuwa Fela Anikulapo Kuti. Kugeuza jina  kulihimiza umuhimu wa desturi za Waafrika. Anasema katika  sinema iliyotengenezwa mwaka 1982 kwamba leo Waafrika hawajui wanakotoka wala wanakokwenda.  “Mwafrika anamwiga Mzungu na katika miaka hii ameshindwa kutunga lolote jipya kutokana na kuiga iga na kutojijua.”
Tunaona aibu kufuata desturi zetu, anasisitiza. Analaumu kuwepo kwa “dini za kigeni” zinazotufanya tusijijue au kujipenda wenyewe.
 Anasisitiza : “Ukristo na Uislamu si dini zetu.  Na tunafahamu sababu gani Ukristo na Uislamu vimeenea bara zima la Afrika. Ni kuwadhulumu watu.  Wakristo wana fikra na tabia  za Waingereza na Wamerakani ilhali Waislamu wana tabia za Waarabu. Lengo ni kutuondoa  Waafrika toka mizizi  na fikra zetu tu.  Waafrika lazima tujijue sisi nani...”
Kufuatana na hesabu zilizofanywa mwaka 2009, Afrika inao waumini wa madhehebu ya kijadi, 137,842, 507. Linganisha idadi  hiyo na Waislamu 371,459, 142 na Wakristo 304,313,880;ilhali  waumini wa dini nyingine (mathalan Wahindu) ni 9,818, 542.  
Dini zinazoongoza barani ni Wakristo na Waislamu. Maswali aliyouliza mwanamuziki Fela Kuti mwaka 1982 yanaweza kuudhi baadhi yetu tunaoamini dini hizi. Lakini bora tujiulize alikua na malengo gani?
Ukichunguza migogoro inayoendelea duniani sasa hivi, masuala ya mabomu na umwagaji damu yanatokana na nguvu za wenye mali na wasio mali, maskini na matajiri. Vita vinapopiganwa au silaha zinapotumika, anayefaidi ni mtengenezaji na muuza vifaa hivyo. Moja ya sababu Fela Kuti alipigwa, mamake akauawa na hatimaye yeye mwenyewe kutiwa jela (hadi alipotolewa mwaka 1986) ilikuwa kukua kwa tawala za kijeshi na kutumia silaha kukandamiza wananchi.
Mbali na silaha zinazouziwa magaidi na wanajeshi wanaobaka wanawake Kongo, Sudan na Somalia sasa hivi pia yapo makampuni makubwa makubwa mfano Microsoft, Motorola, Ford na Cocacola yanayoshirikiana na serikali za nchi maskini  kuhakikisha maslahi ya makampuni haya yanaendelezwa. Zinapotokea fujo,  mapinduzi ya kijeshi, vita nk makampuni  makubwa kama Lockheed huhakikisha silaha zinauzwa.
Mwezi Mei mwaka jana serikali ya Marekani ilikisia dola 9.7 bilioni kila mwezi kuendesha vita vya Afghanistani. Fedha hizi ambazo zingeweza kutumika kuleta maendeleo ya kijamii zinanunulia silaha za sumu. Silaha hizo hizo huuzwa kwa waasi na viongozi mbalimbali Afrika wanaoendeleza vikundi vya kigaidi sasa hivi.
Wakati hali ya uchumi duniani ikiendelea kuwa mbaya (toka kuanza kwa tatizo la mabenki 2008) hali ya wananchi Afrika inazidi kuharibika. Serikali mbalimbali zinaendelea kutawaliwa na wanasiasa wasiowajali wananchi.  Neno demokrasia ambalo lilianza kutumika rasmi 1990 baada ya dhana ya vyama vingi kuingia barani sasa hivi limechuja maana. Katika miaka minane iliyopita hali imezidi kuwa mbaya kiasi ambacho nchi nne zimetekwa na makundi makubwa makubwa ya Waislamu. Nchini  Mali vyama vya Iyad Ag Ghaly ( mpinzani wa serikali toka miaka ya 1980)na Ansar Dine vimechukua theluthi mbili ya nchi hiyo baada ya mapinduzi dhidi ya serikali iliyoshinda uchaguzi halali kupinduliwa. Sharia, itikeli na tabia zinazofanana na zile za  Mataliban wa Afghanistan zimetangazwa: TV,  mpira, kuvuta sigara, pombe haviruhusiwi; wezi  na wahalifu mbalimbali hukatwa mikono au kupigwa mawe; njaa, ukosefu wa umeme na mafuta vimeshasababisha wakimbizi laki mbili.

Mbali na mabadiliko haya kundi hili la Matuareg (ambao walishapigana Libya mwaka jana) karibuni limeharibu magofu ya kihistoria yaliyopo mji maarufu wa Timbuktu.  Timbuktu iliyoanza kuwika sana karne ya 12 ni mahali penye kumbukumbu zinazoweza kufananishwa na Kilwa, Zanzibar na Bagamoyo.
Uchafuzi huu una mahusiano na Al Kaida ambayo hulka yake ni ugaidi. Mahusiano yapo vile vile Nigeria (ambapo Boko Haram huchoma makanisa na kuharibu jamii) na Somalia (Al Shabaab). Vikundi hivi vya magaidi vinachafua  si tu sura na wajihi  wa Waislamu (Uislamu maana yake ni amani), bali pia vinaigwa na kufuatwa hadi Tanzania ambapo karibuni tumeshuhudia uchomaji makanisa Dar es Salaam na Unguja. Je, nini hasa kiini cha tatizo? Je ni dini au jambo zito zaidi?
Tutathmini  zaidi mada juma lijalo. 

Ilishatoka gazeti la Mwananchi....



No comments:

Post a Comment