Monday 7 May 2012

UKEKETAJI WA WANAWAKE WAPIGIWA MADEBE UZUNGUNI

Majuma mawili yaliyopita gazeti mashuhuri  na aghali kuzidi yote  Uingereza- The Sunday Times lilitangaza habari moto zilizopeperushwa duniani kuhusu  akina mama zaidi ya laki moja Uingereza wanaodhalilishwa na ukeketaji. Gazeti hili lililoanzishwa mwaka 1821, lilifanya uchunguzi wa kisiri siri   kufichua waganga wa Kiafrika wanaotoza shilingi milioni mbili za hapa kumkeketa mwanamke mmoja. Kwa mujibu wa BBC wanawake husika  wanatoka  Yemen, Somalia, Eritrea na Ethiopia.
Ona mfano hapa...
  <--more--!>

Mara baada ya uchunguzi kutangazwa mkuu wa maadili Shirikisho la Waganga Uingereza, Profesa Vivienne Nathanson alihojiwa na runinga ya Sky akafafanua kwamba wasichana wenye miaka kumi kuendelea hulazimishwa  kukatwa na ndugu zao wa kike.
Mwaka 2001 shirika la Afya Duniani (WHO) lilikisia wanawake  milioni138 duniani wamekeketwa. Desturi hii iliyojizatiti Afrika, Asia  na Mashariki ya Kati inazagaa leo nchi zilizoendelea kutokana na wahamiaji wanaokimbia  vita na adha nyingine za karne ya 21.
 Alice Walker mmoja wa waandishi weusi mashuhuri aliyeanza kukekemea ukeketaji toka miaka ya 1980...

Awali  wataalam na waandishi wachache (kama Mmarekani mweusi Alice Walker) tu ndiyo waliopiga kelele- ila kutokana na wanawake   wengi kufurika mahospitalini- serikali na vyombo vyake vimeanza kuchachamaa.
Hapa Uingereza sheria kuzuia ukeketaji ilipitishwa rasmi  2003. Sheria  inasisitiza ni uhalifu kukata sehemu zozote  za siri za msichana( ila kwa sababu za kiafya) -hukumu yake jela miaka 14. Vyombo vya habari vinalalamika toka sheria  ilipopitishwa  hakuna yeyote aliyeshtakiwa.
Sababu kuu ni kwamba familia na ndugu za wasichana wanaokeketwa huchukuliwa kimya kimya kwao wakapasuliwa na kurudishwa bila mkono wa sheria  kufahamu. Profesa Vivienne Nathanson anasisitiza kuwa serikali husika Afrika na Asia zinabidi kusaidia kufuatilia mbali kero hii.
Lakini wahusika wenyewe wanasemaje?
Mmoja wa kina mama wa Kisomali aliyekeketwa akiwa na miaka mitano tu- Waris Dirie- anayefahamika sana duniani baada ya miaka mingi kama mtangazaji wa mavazi na uzuri (“model”) kawa mstari wa mbele kuupinga. Toka 1997 Waris ni balozi wa Umoja wa Mataifa akiongoza kampeni hii.

Waris (juu na kitabu chake kinachoelezea mada hii) aliiambia Sunday Times: “Kama msichana wa Kizungu akiumizwa – polisi  mara moja huuvunja mlango. Lakini msichana Mweusi akikeketwa hakuna anayejali. Huu ni ubaguzi wa rangi.”
Je ukeketaji ni nini hasa?
Unapoongea na baadhi ya wananchi hapa na nyumbani wanaelewa ukeketaji kama  tohara ambayo wanaume pia hufanyiwa. Mwanaume anapotahiriwa  haumii wala kuugua baadaye- ilhali mwanamke huteseka maisha yake yote.
Watetezi wa ukeketaji wanasema jadi imekuwepo maelfu ya miaka kabla  ya dini za Kiislamu na Kikristo.
Wataalamu wamegawanya ukeketaji au FGM (“female genital mutilation”)  sehemu nne. Mosi ni kukiondoa kinembe ili kufifisha hisia  za mwanamke. Wanabailojia wanatuambia kwa wanawake kiungo hiki  ni sawa na uume wa mwanaume. Aina ya pili ni kuondoa kiungo hicho na mashavu au nyama zinazouzunguka uke. Aina hii ya upasuaji ndiyo iliyoenea zaidi- na kama ile ya kwanza ina lengo la kupunguza kabisa hisia za mhusika. Ya tatu  huondoa  midomo ya uke na kuishona. Baadaye hubakishwa tundu dogo tu kupitisha mkojo na damu wakati wa hedhi. Tatizo hufika wakati mwanamke akiwa katika siku zake au wakati wa mimba na uzazi. Wasichana ambao bado hawajawahi kuzaa hupata shida zaidi maana damu ya hedhi haitoki sawasawa na huziba.  Aina ya mwisho ya ukeketaji (tunaelezwa na waganga waliowatibu kina mama waliohudhuria hospitali za Uingereza ) inahusu kuondoa nyama nzima ya uke na “kuingiza vidude mbalimbali vinavyosababisha maumivu makali.”
Idadi ya wanawake  hospitali za Uingereza iliongozeka  toka 109  mwaka 2003 hadi  wagonjwa 317 mwaka 2007. Kati ya matatizo ya msingi yanayowafika wanawake hawa ni haja ndogo kuchukua wastani wa dakika 20 msalani kutokana na njia au shimo la mkojo kuziba. Pili, badala ya hedhi kuchukua siku saba wahusika huendelea siku  28 kutokana na mfereji mdogo uliosababishwa na ukeketaji.
Alipohojiwa dada mmoja wa Sierra Leone alidai ukeketaji humfanya mwanamke “awe msafi na mwenye afya.”
Miaka ya karibuni, Heartlands, zahanati maalum iliyoundwa na mkunga  wa Kiingereza Alison Byrne, kusaidia wanawake wanaoteseka mjini Birmingham  huhudumia wanawake kwa kuwapasua, kuwashona upya, kuwapunguzia maumivu.
Tatizo haliko Uingereza tu.
Niliongea na mwanamke mmoja wa Sudan aliyekimbilia nchi za Scandinavia. Mumewe alikuwa mfanyabiashara aliyesafiri Uarabuni. “Kila akiondoka ilibidi nizibwe nisilale na mwanaume mwingine. Akirudi nyuzi ziliondolewa. Nikishapona naanza kufanya naye tena mapenzi. Nikiwa mja mzito na nikishajifungua- nazibwa tena. Mtoto akikua nikitaka tena kujifungua mwingine nazibuliwa tena. Mume akisafiri nashonwa tena.”
http://www.youtube.com/watch?v=pPJEl-gyQOo
Matokeo leo kukaa au kulala shida- licha ya haja ndogo au shughuli nyingine za kibinadamu. Ilimbidi atorokee Majuu ambapo  anatibiwana mumewe kaapa akimkamata atamuua.
 Ukeketaji unapigwa vita Majuu. Mitandao kadhaa imefunguliwa kusaidia mathalan- “Digital Spy Forum” uliochapa  barua hii Jumapili ya tarehe 22:
“Ukeketaji wa wasichana  ni sawa namna jadi ilivyotumika kufunga miguu ya vigoli zamani China kusudi wasitembee- ikasababisha maumivu yasiyosemekana, vifo vya mara kwa mara na vilema vya kudumu.”
Mwingine- Emily 222 akauliza:
“Lengo la mila hii ni kuwataka wasichana wawe safi kabla ya kuolewa sio? Je ina maana Mungu alikosea kuwaumba wachafu walipozaliwa? Je, Mungu alikosea kuwapa wanawake viungo sawa na vya wanaume kusudi wasifurahie ngono? Kinachoudhi zaidi ni namna mama zao hawa wasichana wanavyoendeleza mila hii. Huu ni udhalimu kwa watoto.”
 Mwalimu Nyerere akiwa na Rais Barre wa Somalia miaka ya Sabini...Nyerere alikuwa kiongozi wa Afrika aliyepinga mila hii...

Hapa Bongo mikoa 19 inaendeleza ukeketaji uliopingwa  zamani na marehemu Mwalimu Nyerere. Wapo wanawake wanaotetea na pia wanaume wanaosema ni jadi muhimu. Wanaume ambao wamewahi kuwa na wanawake au wapenzi waliokeketwa hawana maoni mazuri. Mmoja aliniandikia:
“Niliwahi kuwa na Msomali, Mburundi na Mswahili ambao wote wamekeketwa. Ilibidi niachane nao maana wakati wa kufanya mapenzi ni dhiki tupu- hawasikii lolote. Baadaye nikagundua hata kwa wanaume wa Kisomali kijadi kufanya mapenzi ya kimwili si muhimu. Hufanya tu mara moja kwa msimu – kupoteza tu siku kwa kutafuna mirungi badala ya kufikiria kama sisi wengine ambao ukiwa na mwanamke kukutana kimwili ni mojawapo ya mapenzi ya kila siku. Nilishindwa.”
Jadi hii inayotukuza mateso kama “utamaduni” wetu inaweza kufananishwa na  mauaji ya Albino kutumia miili yao kama suala la bahati, ushirikina au mali. Si tu dhambi bali hudhalilisha wanawake wetu walio sehemu mahsusi ya uzalishaji mali na wanadamu (uzazi). 
 Ilichapwa Mwananchi Tanzania Jumapili 6 Mei, 2012.

No comments:

Post a Comment