Showing posts with label Historia. Show all posts
Showing posts with label Historia. Show all posts

Sunday, 27 November 2011

MACHALARI MGOMBANI MOSHI NA NYAMA CHOMA ZA ARUSHA


Dunia yetu ina kila aina za udongo.
Udongo wa Mpirani nje kidogo ya Moshi mjini unanikumbusha wa Kigoma ambapo rangi yake inakurubia wekundu. Mimea ya Mpirani ni migomba, mapera, machungwa, ndimu, maembe, kahawa na gari analoendesha dada yangu Juliana linakwenda taratibu, likikwepa mashimo shimo ya udongo huu.


“Unaona ule msikiti?” naulizwa. Nikiwa mdogo haikuwepo misikiti mashambani Moshi.  Kidesturi migombani kwa Wachagga hujazana makanisa.
“Wapo mangi wengi Waislamu siku hizi,” dereva anafafanua.
<--more--!> 

Sunday, 10 July 2011

SOMO KUTOKA MAISHA NA KIFO CHA MWANAMUZIKI GIL SCOTT-HERON

Je, pana faida gani kusikiliza habari za Mmarekani mweusi Gil Scott- Heron aliyefariki mwezi uliopita? Sidhani wapo Watanzania wengi seuze Waafrika waliomjua msanii huyu aliyetoa albam 15 za muziki na vitabu vitano; vitatu vya mashairi na riwaya mbili alizochapa akiwa bado shuleni. Gil Scott- Heron alipofariki Ijumaa Mei 27 akiwa na umri wa miaka 62, alibeba taji la mwasisi wa muziki wa Hip Hop na “Bob Dylan Mweusi.”
Gil Scott-Heron akitumbuiza na bendi yake "Amnesia Express" ukumbi wa Jazz Cafe, London mwaka 1999. Picha na F Macha
<--more--!>

Wednesday, 30 March 2011

KITABU KINACHOELEZEA YALIYOWAFIKA WAPINZANI TANZANIA CHATOKA UINGEREZA...

Kina kurasa 272.
Toka nchi yetu iwe huru miaka hamsini sasa hajatokea Mtanzania akaandika kitabu cha aina hii.  Watanzania tunaogopa. Hofu hiyo imeenea miaka mingi na imetushika hata sisi wanahabari wenyewe.
<--more!-->

Sunday, 30 January 2011

MTINDO WA KISASA WA NYWELE UNAHARIBU AFYA ZA WANAWAKE WEUSI

Watu wa kabila la Chwi kule Ghana wanaozungumza lugha iitwayo Tshi wana methali kuhusu umuhimu wa kupendeza. Inashauri: “Ikiwa mwenda wazimu ataiba nguo zako na kukimbia nazo wakati wewe uko majini unaoga, itakuwa vyema utafute angalau kipande cha kitambaa ujifunge wakati unamkimbiza maana usipofanya vile watazamaji watadhani na wewe umeheuka.”
Hakuna mwanaume ambaye hajawahi kupayukiwa kuwa asuburi wakati ndugu yake wa kike anajipodoa akijiremba. Na kati ya mapambo yote nywele zinaongoza foleni. Mwanaume waweza kutoka bila kuchana nywele, unaweza ukawa nusu kipara (kama mimi mwandishi) lakini hujali mradi u msafi utatoka zako mitaani. Kwa mwanamke kujisanifu nywele ni tendo muhimu sana. Ndiyo maana waandishi mbalimbali wa hadithi hawakosi maelezo ya ususi ndani ya riwaya zao.

Monday, 17 January 2011

MECHI YA ARSENAL UWANJA WA EMIRATES LONDON...

Niko uwanja wa Emirates, kaskazini ya London.
Ili kuingia hapa yabidi tukae foleni ndefu iliyoanzia milango mikubwa inayolindwa na askari doria juu ya farasi. Ingawa baridi ya leo kali wale askari wamesimama macho makali wakituangalia kama siafu tayari kung’ata. Si Arusha, si London; askari ni askari.
Emirates iko kitongoji cha Islington. Miaka yote niliyoishi mjini London huzijua mechi za Arsenal  maana si mbali  na ninapoishi; jirani na Tottenham Spurs maadui mwitu wa Arsenal. <!--more-->
Huu ni msimu wa barafu linalodondoka kama mvua ya manyunyu. Kila mmoja wetu kavalia makoti mazito, fulana mikono mirefu, kofia zilizofunika vichwa, masikio  na leso nzito za kukinga shingo na vifua. Mikono imefunikwa kwa maglavu ya sufu na baadhi ya ajuza waliokuja mpirani wamebeba mikongojo wasiteleze. Kila tunapokanyaga  kelele za Kocho! Kocho! Kocho! juu ya kokoto la barafu zinasikika maana tumevalia mabuti makubwa ya msimu huu wa kutisha Ulaya.
Mara nakumbushwa zamani nikikulia mgombani Moshi na Arusha  miezi ya masika. Mbali na matope na utelezi, zilipita nyungunyungu na konokono. Mvua za nyanda za juu Afrika hutaabisha magari na wakazi wake; ila maisha hayasimami. Ndivyo pia Uzunguni; ingawa barafu ni ukiwa mtupu, binadamu hawaachi kwenda kazini wala stareheni.
Si ajabu basi hapa Emirates, wapo pia watoto, mama na baba zao ; hata mababu wakipambana na ubaridi mkali unaojaribu kila njia kupenyeza mavazi tuliyojigubika.
Ingawa foleni ni ndefu, utaratibu wa Kizungu ni kupeleka mambo haraka. Huwezi kuja hapa bila tiketi, kwa hiyo mpango uliopo ni kuonyesha tu nakala uliyoshanunua mtandaoni ikakatwa nusu, kisha ukaelekezwa kwa askari wanaokagua. Nje haparuhusiwi kabisa wauza tiketi za magendo au wamachinga; macho ya askari na kamera za video zinachunguza kila kitu...
Ukishapita foleni huruhusiwi kuingia na chupa, kinywaji au kisu. Ukishapekuliwa unapita na kujikuta ndani ya vyumba vikubwa vya kuingilia uwanjani. Vyumba hivi vina mabaa na mijigahawa inayouza vitafunio, vinywaji, bendera na skafu za rangi nyekundu na nyeupe; rangi rasmi za timu ya Arsenal. Ukitaka kuingia na bia unalazimishwa uimimine ndani ya bilauri za plastiki. Hii ni kwa usalama; zamani watazamaji walikuwa na tabia ya kuwatupia wachezaji vyupa.
Ewalla.
 Ninapoingia vyoo vya Emirates nakumbuka mwaka 1988 nilipotazama mechi ya Brazil na Argentina uwanja wa Maracana mjini Rio De Janeiro. Alicheza pia mwanasoka maarufu, Diego Maradona. Kwa kuwa Brazil na Argentina ni kama paka na mbwa; ilikuwa vigumu kwangu na wenzangu  kumshangilia Maradona. Kila alipogusa mpira, Wabrazili walimzomea. Sisi wachache tulimshangilia  alivyosakata chenga za kipekee. Wakati wa mapumziko tuko chooni; likaja kundi la Wabrazili.
“Nyinyi mnashangilia Argentina?” Akauliza mmoja, kwa Kireno.
“Hapana, tunamshangilia Maradona,” Mmoja wetu akajibu.
Mwingine akaongeza. “Anacheza kama Pele!”
“Mtusamehe hatujawahi kumwona mchezaji mahiri hivi,” Nikafafanua kiangalifu.
Pale msalani pakawa kama pamedondoka bonge la joka.
“Sikilizeni! Mkitaka kutoka hapa salama leo basi muache upumbavu wa kuwasifia hawa washenzi !”
Kilikuwa kitisho bab kubwa. Hadi leo nikiwa vyoo vya viwanja vya mpira nakikumbuka.  Ila hapa Emirates mambo tofauti; washabiki wa Arsenal wako vyoo vya upande mmoja na wa upinzani mwingine; hakuna maadui kukutana.
Tumo, tumo...
Emirates iliyofunguliwa rasmi mwaka 2006, ina nafasi ya watazamaji 60, 355 ambapo Old Tafford wa Manchester United ni 75,957.
Timu ya Arsenal ilianzishwa mwaka 1886 kitongoji cha Woolwich Arsenal ambapo siku hizi pamebakia tu jela maarufu ya Belmarsh. Mwaka 1913 ilihamishiwa kaskazini baada ya wafanyabiashara kugundua sehemu hiyo haikuvutia wateja. Arsenal ni timu pekee iliyowahi kucheza misimu miwili mfulululizo bila kufungwa na klabu yeyote, mwaka 2003 na 2004. Kitendo hicho kilichowakatia jina la “Invicibles” kimewahi kuonyeshwa na timu moja tu katika historia ya ligi ya Uingereza; yaani Preston mwaka 1888 - 1889.
Uwanja unanguruma.
Nipo karibu na walipokaa ustaadh Arsene Wenger na makocha wapinzani wa Wigan.
Jambo muhimu unalogundua ukikutana na watu mashuhuri ni jinsi walivyo tofauti na vile tunavyowadhania. Nilipokuwa Bongo nilijiuliza kwanini wachezaji wetu wa kitaifa wadogo vile kiumbo?
Lakini ninapokaa hapa nikiwaangalia Samir Nasri, Theo Walcott,  Cesc Fabregas na hata kocha mwenyewe, Wenger, nashangaa walivyokuwa pia wadogo wa umbo.
Mpira umeanza.
Watazamaji wanaimba:
“Red Army! Red Army!” (Jeshi Jekundu); huku Wigan ikijaribu kila njia kuzuia kipigo. Natetemeka kwa baridi; uwanjani barafu linaanguka. Namwangalia golikipa wa Arsenal (mwenye jina gumu), Wojciech Sczcesny, akiruka ruka ajipe joto. Hana kazi kubwa leo maana washambuliaji wa Wigan hawajapata mwanya. Ghafla Eboue kachomoka; kampa pasi Fabregas; Fabregas katoa ukanda kwa Theo Walcott anayekimbia kijogoo. Mpira wa kupendeza; lakini Walcott kategewa kaanguka.
Uwanja mzima : Aaaaaah!
 Baada ya dakika kumi na tano bila bao lolote kufungwa watazamaji wanaanza kuimba kwa nguvu:
“You dirty northern northerners!” (Nyinyi wapumbavu toka kaskazini), maana Wigan kwao kaskazini ya Uingereza.  Mpira unaendelea hadi mapumziko bila bao lolote. Wakati wachezaji wakienda kupumzika, wimbo maarufu dhidi ya maadui wa jadi unarindima:
“Stand Up If You Hate Tottenham!” (Simama kama unaichukia Tottenham)! Kila mtu anasimama.
Ila kinalonishangaza ni namna starehe ya mpira ilivyobadilika. Miaka ishirini iliyopita niliwahi kutazama mechi ya Liverpool. Nakumbuka namna wanaume walivyolewa wakitafuta ugomvi.
Leo Emirates wamejazana wanawake, watoto, wazee; kifupi, familia. Wapo vigoli waliokuja peke yao kama Joanna, Mmarekani anayepiga picha.
“Vipi ? Unafurahia mechi?” Namuuliza.
“Sana. Mi lakini mshabiki wa timu ya wanawake wa Arsenal. Nampenda sana Kelly Smith.”
Timu ya wanawake ya Arsenal ni klabu bingwa kushinda zote Uingereza. Iliundwa mwaka 1987 na imeshatwaa vikombe 33 vikiwemo ligi za kitaifa za wanawake na Ulaya (UEFA). Kutokana na ufundi wake Kelly Smith ambaye (mshambuliaji) ni mchezaji wa timu ya taifa ya wanawake Uingereza, kaitwa Zinedine Zedane wa kike.
Mapumziko yamekwisha.
Mechi inaendelea na  mwisho Arsenal wanashinda kwa mabao mawili. Wakati tukipambana na “tope” lile la barafu watazamaji waliohamasika wanaimba wimbo :
“Who are you? Who are you?” (Nani wewe)
Natetemeka baridi nikikimbia na wenzangu. Najiuliza vipi wale wachezaji walimudu kucheza dakika tisini ndani ya barafu? Ama kweli kila mtu na ajira yake.

 -London, Jumanne, 11 Januari,  2011

Ilitoka Mwananchi, Jumapili 16 Januari, 2011.

http://www.mwananchi.co.tz/mwananchi-jumapili/38-johari/8405-nipo-ndani-emirates-wa-arsenal

Sunday, 9 January 2011

KUJIENDELEZA, MAZOEZI NA KUINUA VYUMA -Sehemu ya Mwisho

Makala kadhaa zilizopita zimesisitiza sisi wananchi wenyewe kujiendeleza. Lengo la insha hizi ni kukumbusha wewe mwananchi kwamba huwezi kusonga mbele bila elimu na maarifa sahihi; kwamba maendeleo yanawezekana.
Jamii ya Marekani imejenga utamaduni huu uitwao Self Help. Ni utamaduni uliozalisha biashara ya vitabu, video, magazeti na vipindi mbalimbali vya runinga vinavyosisitiza mwananchi kujituma badala ya kutegemea uchawi, dini au imani nyingine peke yake. Lengo ni kuweka nguvu za kimaendeleo mikononi mwa mwanadamu. Kelele inayopigwa ndani ya utamaduni wa Kimarekani ni kuwa lolote linawezekana kwa anayejitahidi.

Sunday, 2 January 2011

MAAZIMIO YAKO 2011 YAWE KUJIENDELEZA KIFIKRA...

Kabla ya kuendelea na mada ya mazoezi tuliyoiongelea Jumapili iliyopita tuutazame mwaka mpya 2011, kijasiri. Msomaji huenda hufurahishwi na hali ya uchumi, wanasiasa wanaotuongopea na maisha yanayoendelea kuwa  magumu.
Hisia hii imeenea ulimwenguni. Imekithiri kiasi ambacho kuna fikra mwisho wa dunia unakuja. Wapo wanaoeneza falsafa kwamba mtabiri wa zamani Nicodemus aliambiwa na Yesu Kristo kuwa dunia itakwisha 2012. Mfano mzuri ni blogu la “2012 Doomsday Prophecies” (Tabiri za Siku ya Kiama 2012) linalonukuu Biblia (Yohanna Sura ya 3:8) na hali ya mafuriko, matufani na matetemeko makubwa miaka hii (Haiti, 2010) kama ishara ya angamio hilo.
<!--more-->
 Bila shaka msomaji umesikia namna msimu wa barafu ulivyokuwa mkali Ulaya na Marekani. Usafiri umeathiriwa, watu 60 walifariki mwezi Desemba nchini Ujerumani, Urusi, Ubeljiji na Poland. Viwanja vya ndege vimedhurika na safari kuvunjwa.
Blogu la “Doomsday” linapiga makofi kusifia ukweli wa tabiri zake Nicodemus. “Doomsday” linatukuza kalenda ya Maya inayosisitiza mwisho wa ulimwengu na mwanzo mpya...
Barani Afrika, leo, imani kuwa uhai umelaaniwa zimeshika hatamu. Kutokana na maafa ya vita, magonjwa ya UKIMWI na malaria, Waafrika wengi waliodhalilishwa na viongozi waongo wanaowaibia na kuwadanganya kila siku wamekimbilia dini. Imani zetu za jadi ambapo mababu na mabibi zetu walitambikiwa na kuaminiwa  zimetupwa shimoni. Badala yake wengi tuko tayari kupigana hadi kufa kutetea dini zilizoletwa na wageni miaka michache tu iliyopita. Dini hizi zinazotukuza upendo, amani na Mungu kuwa suluhisho zimekuwa ndiyo ahueni ya mawazo na hisia. Kimsingi wanadamu dunia nzima tunaupokea mwaka 2011 kwa utata.
Je, ni kweli mwisho wa dunia utakuwa 2012?
Mwezi ujao natimiza miaka 56. Toka nikiwa mtoto nimezisikia hadithi hizi za mwisho wa dunia. Mwaka 1962 nikiwa darasa la kwanza hofu iliyoenea ilikuwa bomu la Atomiki na vita vikuu vya tatu vitakavyotokea kutokana na uhasama baina ya Wamarekani na Warusi. Uhasama uliota kichuguu wakati Rais Fidel Castro wa Cuba na makamu wake Che Guevara walipoamua kumwambia Mmarekani afilie mbali, asiendelee kuonea mataifa na watu maskini. Mgogoro wa Cuba na Marekani, 1962, uliitisha dunia nzima. Na haukuwa wa kwanza miaka ya Sitini. Uliendelea Vietnam, Kongo na hata Zanzibar. Kila mahali wanadamu walipojaribu kudai haki zao toka ukoloni na hali ngumu kiuchumi walitishwa na tembo wawili yaani Urusi na Marekani.
 Kipindi chote nilichosoma shule ya msingi hadi naingia sekondari 1969 kilikuwa cha hofu ya bomu la Atomiki; kwamba dunia italipuka dakika yeyote. Tukiwa watoto habari hizi zilichanganya migogoro ya kivita Vietnam, mauaji ya viongozi mashuhuri  Rais John Kennedy wa Marekani (1963), Malcolm X (1964), Martin Luther King (1968) na Waziri Tom Mboya wa Kenya aliyepigwa risasi mjini Nairobi, 1969.
Miaka ya Sabini ilizidi kuchubua.
 Kila mahali wanadamu walidai haki zao, wakipingana na tawala zilizowatesa. Hapa Bongo migomo ilitokea viwandani, mashuleni na moja ya mambo makubwa  ni kuuawa kwa  Rais wa kwanza Zanzibar, Abeid Amani Karume, mwaka 1972. Bara zima la Afrika lilichachamaa  na wapigania Uhuru, Angola, Msumbiji, Namibia, Zimbabwe, nk. Nchi zilipinduliwa  na lililotuathiri zaidi Wanabongo ilikuwa Jemadari Idi Amin Dada aliyemtoa Rais Milton Obote madarakani  Uganda, mwaka 1971.
 Kilichonguruma zaidi ni Wapalestina. Wanaharakati waliteka nyara ndege wakidai kutambuliwa; huku nyuma nchi tajiri za Kiarabu zilizotoa petroli zikipandisha bei mafuta hayo kuwakamua matajiri wa Ulaya na Marekani walioisaidia Israeli dhidi ya Wapalestina. Hapa ndipo mgogoro uliopo leo Mashariki ya Kati na Afghanistani ulipoanzia. Ndege zilitekwa nyara na tatizo la Wapalestina likajulikana. Wakati haya yakiendelea  hali ya uchumi iliharibika kiasi ambacho nchi tajiri zilipunguza kabisa bei za mazao toka nchi changa. Uchumi mgumu tulionao leo ulikuwa pia taswira ya miaka ya Sabini. Kiama kilizungumziwa. Fasihi na sanaa vilijitahidi kuliwaza. Mwanareggae Bob Marley, toka Jamaika, aliimba kuhimiza mapenzi, amani na harakati.
Miaka ya Themanini iliangukiwa na UKIMWI. Mwanzoni UKIMWI ulisemekana tu  tatizo la wasenge. Ila mwaka 1987 UKIMWI ulienea hata wasiokuwa firauni. Afrika Mashariki UKIMWI ulikatiwa jina la SLIM kutokana na jinsi ulivyokondesha walioupata. Miaka ya Themanini na Tisini uliwapa Waafrika imani kuwa bara letu limelaaniwa. Laana iliraruka  mwaka 1994 kutokana na mauaji ya Watusi na Wahutu, laki nane, Rwanda.
Kiulimwengu miaka ya Tisini ilikuwa ya mauaji ya jumla jumla. Aprili 1995 mji wa Oklahoma, Marekani, ulistuliwa na gaidi Timothy McVeigh, aliyejeruhi 680, akaua   168, (kati yao watoto 19) na kuharibu majengo 324 kwa mabomu. Ni kipindi hiki kila mtu alipoongelea mwisho wa dunia yaani 1999 kuangukia, 2000. Mwanamuziki  wa Kimarekani, Prince alitunga wimbo uitwao 1999.
 Ugaidi na mabomu ya Waarabu walioudhiwa na siasa za Magharibi kuhusiana na Wapalestina wakiongozwa na Al Kaida ya Osama Bin Laden yalisambaa kuanzia Dar es Salaam (1998) hadi New York, Septemba 2001.
Kifupi hakuna kipindi chochote nilichoishi ambapo hapakuwepo  fikra kwamba mwisho unakuja. Ukishunguza historia yetu wanadamu kila kipindi  kimekuwa na vita au machafuko ya mazingira.
Msomaji zingatia kwamba masha yetu ni mseto wa mabadiliko, mvutano wa maumbile, mabaya na mazuri, moto na baridi, jike na dume, matajiri na maskini, wenye uwezo na wasio uwezo.
Je, utamuduje?
Mwaka 2008 nilimhoji mwanasaikolojia wa Kiingereza, Dk. John Conolly, pia mganga wa wenda wazimu. Alisema wagonjwa wa vichaa wanaongezeka duniani kutokana na baadhi yetu kushindwa kuyaelewa maisha ili kuyamudu. Alishauri kila mtu kujiuliza maswali akiamka au akienda kulala.
Unapoamka jiulize je, leo nitafanya jambo gani kujiendeleza kitaaluma?  Je, nitafurahishaje nafsi yangu? Na kama sina raha nitachukua hatua gani kukabili na kutawala mazingira na maisha yangu badala  ya kuyahofia?
Je Watanzania wangapi wanaazimia kununua kitabu mwaka huu kujisomea? Idara ya Elimu ya Umoja wa Mataifa mwaka jana ilikiri kwamba watoto 72 milioni duniani hawasomi;  na kwamba elimu ni tatizo mosi la jamii maskini ulimwenguni.
 Fidel Castro wa Cuba anasema katika kitabu cha maisha yake kuwa tumeumbwa kuuendeleza ulimwengu wetu. Tuko hapa tuwazae wanadamu wengine watakaochangia uhai.  Hivyo basi, mwaka 2011 uwe wako kujiendeleza, ndugu msomaji.

 -London, Jumanne, 28 Desemba,  2010.


Ilichapishwa gazeti la Mwananchi, Jumapili, Januari 2, 2011.


http://www.mwananchi.co.tz/mwananchi-jumapili/38-johari/7961-maazimio-yako-mwaka-2011-yawe-ya-kujiendeleza-kifikra