Sunday 7 June 2015

KWANINI LEO WAZUNGU WANAHUSUDU MAMBO TUSIYOYAJALI TENA?


Yupo Mwingereza mmoja maarufu sana aliyetimiza miaka 40 mwezi jana.
Huyu jamaa ana kipindi chake katika TV anachodondoshwa mwituni, jangwani au vichaka vya sehemu mbalimbali za dunia  na kuachwa. Hukaa bila chochote bali kisu kikali, mfuko mdogo na nguo alizovaa. Kuna wakati aliachwa pori moja la Zambia. Huko alizingirwa na wanyama, mito, chemchemi na nyika tupu. Alilala juu ya mbuyu. Chakula  kilikuwa wadudu, nyoka na maji ya mvua. Na hii tabia yake ya kula chochote anachokiona nyikani kiwe buibui,  chura, mchwa, asali, nyungunyungu,mbegu, matunda, madafu, majani, panya, fuko au ngiri ina malengo na mafunzo.
Mosi anajaribu kuonesha namna wanadamu tunavyopaswa kujua kuishi (na kumudu) bila kukata tamaa iwapo majanga yakitutokea au hakuna namna. Pili, anasisitiza wanadamu, (hususan Wazungu) tumeichangamkia teknolojia tukapoteza ubunifu, tukawa wavivu na waoga wa mazingira. Tatu, huelekeza kutokata tamaa, kujitegemea na kuwa wajanja pale shida yeyote inapojitokeza.  Zamani nikiwa jeshi la kujenga taifa (JKT) tulifundishwa ujuzi huu uliobatizwa nahau : “Ujanja wa Porini”...
Jina la huyu “mbabe” anayezidi kupendwa na hasa watoto na vijana  ni Bear Gryllis.
Ujanani, Bear Gryllis (pichani ) alikuwa  askari wa kikosi maalum cha Uingereza.


Bear Gryllis. Picha ya Wikipedia 

WAZUNGU WANAREJEA MAMBO YALIYOKUWA ASILIA YA WAAFRIKA ZAMANI



Mwafrika mwenzangu umegundua nini jipya miaka ya karibuni?
Ukichunguza utaona maradhi yaliyokuwa yakiwang’ong’a  wazee, leo yanaua vijana. Ugonjwa wa moyo, utasa, mapafu dhaifu, uume tata,  uchovu kila mara bila sababu, kisukari, chafya upitapo kwenye vumbi, magari au moshi wa sigara; kiharusi, nk. Maumbile na mazingira yana sheria kali sana. Tusipoyaheshimu hutufunza adabu. Je, kweli tunayaona? Maana sikio la kufa halisikii dawa...
Matokeo nini?

URASTA SI BANGI, UKAIDI, UCHAFU, UHUNI WALA UJAMBAZI



Ethiopia imeelea ndani ya habari za kimataifa  wiki hizi mbili.
Jumapili iliyopita wanawake watatu  wa Kihabeshi  walishinda  mbio za Marathon hapa London. Zilishirikisha wakimbiaji 38,000, wengi  wananchi wa kawaida ( wasio  wanariadha wa kulipwa);  mataifa mbalimbali. Baada ya ushindi “ wanariadha hawa wenye fahari” walipeperusha bendera rangi kijani, manjano na nyekundu. Bendera hii ya Ethiopia iliyosanifiwa mwaka 1897  imekuwa  kielelezo maarufu cha Umoja wa Waafrika na watu weusi duniani zaidi ya miaka mia moja sasa.  Wekundu ni nguvu na imani, kijani ardhi na manjano, kanisa. Tufasili hili kifupi.


 Mwanamuziki maarufu wa Reggae kutoka Ivory Coast, Alpha Blondy. Picha ya Reggae Ville.