Showing posts with label Maisha. Show all posts
Showing posts with label Maisha. Show all posts

Sunday, 20 February 2011

OMBA OMBA NA WALEVI WA KIKE MITAANI LONDON...

Niko dukani nimepanga foleni. Hakuna kitu kinathaminiwa nchi hii ya Waingereza kama foleni. Mara nyingi huwaona wageni waliofika jijini London toka nchi zisizozoea kujipanga. Utamkuta mtu wa aina hiyo akivuka mstari, kabla hata hajaingiza mkono kutoa pesa alipie wenyeji watampigia kelele.
“There is a queue!” (Ipo foleni).
Basi nimo.
Mbele yangu kuna mama mmoja kibonge, tinginya, umbo la gunia. Kibonge nakwambia; mweusi, mchangamfu, sauti kubwa; ana lafidhi ya Kiingereza cha Kijamaika kinachoitwa Patois (tamka Patwaa).
Mwanamke huyu mcheshi ananikumbusha kina mama wanaouza bidhaa sokoni mjini Mbeya. Wakubwa wakubwa, waliojaa bidii, wachapa kazi.
Kabeba vyakula mbalimbali na vinywaji kama wiski na bia ya tangawizi wanayopenda Wakaribian. Wakaribian ni watu weusi toka visiwa kama Jamaika, Trinidad, Grenada, Haiti, Cuba, Montserrat, Barbados, nk. Wamejazana Uingereza. Zamu yake sasa; anapayuka:
“Duu! Nimesahau pesa nyumbani.”
Mwenye duka ni Mhindi toka Sri Lanka.
“ Paundi 25!”
(Kama shilingi elfu sitini).
Mama Gunia, gubeli, bado anafukua pochi.
Anasonya. “ Ah, hizi hapa! “
Anatoa pesa akicheka.
“Nna pesa ! Nna pesa! Unadhani sikuwa na pesa bwa’ mdogo? He! He! he!”
Shere nyingi; analipa, hatimaye. Wapo wanaotabasamu; wapo wanaoudhiwa na vigimbi vyake. Jiji hili huwa na kila aina ya mijeledi. Ni saa tano asubuhi walakin mama keshauchapa. Kinyume na walevi wengine kabeba viazi vikuu, magimbi, ndizi mbivu za manjano kubwa ambazo baadaye atazikaanga (Wakaribian huziita “Plantain”). Sasa n’naongozana naye maana anakaa mtaa mmoja nami. Kachangamka, bado anabonga, utadhani redio.
“Nimeshakaa nchi hii miaka 50! Nilikuja hapa mwaka 1960! Wakati huo weusi tulifananishwa na majibwa. Kuna sehemu ukipita Wazungu wanakupiga kama mwizi. Ilikuwa nisome miaka miwili kisha nirudi kwetu; nikasomea uuguzi, nilipomaliza sikurudi tena.”
Kwanini?
“Ah, nlikutana na brazameni ulimi wa sukari akaniloanisha mapenzi.(Anacheka kwa nguvu) Baadaye wakazaliwa watoto. Sasa wote washakuwa watu wazima, wamezaa, miye nakula maisha tu.”
Tunakumbana na yule dada niliyewaeleza juma lililopita; mnamkumbuka, Vivian? Bado yuko pale pale tulipomwacha; bado anaomba hela, nje ya benki ya Barclays.
Kavalia ile ile suruali yake ya Jeans iliyoshapauka yenye matundu na mabaka mabaka meusi kama masizi. Bado kavalia viatu vyake vile vile vya raba ya Tennis nyekundu vilivyofungwa kwa kamba chafu nyeusi; awali zilikuwa nyeupe sasa hazieleweki. Tena bado anajikuna kuna mapele makubwa mekundu usoni. Ananyoosha mikono yenye kucha ndefu chafu akimpungia Mama Kibonge.
“Queeeen Mary!”
Kibonge anamchekea.
“Yes, Vivian.”
Wanatazamana. Omba omba kakaa pale chini kajikunyata, akipigwa baridi ya Ulaya, Queen Mary (Malkia Maria) anapekua begi lake. Anatoa mkebe mmoja wa bia; anamkabidhi Vivian.
Utadhani Vivian kajengewa nyumba mpya maana tabasamu anayoitoa anapokiona kile kikopo cha bia, maalum! Ajabu pamoja na kuvuta fegi, kulala nje na kuogelea katika ulevi bado meno yake masafi meupe. Ama kweli! Mungu hupambana na shetani; hachafui vyote.
Tunaendelea na safari.
Malkia Maria bado analonga na kutoa mastori, kila baada ya hatua haachi kumsalimia mtu, kumpungia yule kule, akicheka kwa nguvu; juu yake ongezea ile tabia yake ya uchangamfu na nishai ya adhuhuri; basi nadhani wasomaji mnamwona.
“Ungegombea ubunge, Queen Mary,” namkoga.
Anabanja ghafla.
“Bwa’ mdogo. Wakiniona wanadhani mi mlevi; jimama jizee linene, kwisha kazi. Hawan’jui. Siku hizi watu humu mijini hawaangalii watu wakoje; wanaangalia tu walivyovaa wanavyotembea, wakawasema wako hivi na hivi. Ukitaka kujua kitabu kizuri usiridhike na jalada. Kifungue ukisome.”
Anacheka na kubanja tena.
“Nishapitia kila kibaya na kizuri. Nilipohama kwetu nilisemwa, mtoto wa kike nakimbiliaje Ulaya? Nikawaambia wazee msijali, n’najua ninachokifanya. Nilipofika hapa sikuwasahau nyumbani. Baada ya kuhitimu masomo ya unesi nikawa natuma pesa nyumbani. Ilikuwa nirudi lakini bahati mbaya nikakutana na yule mshikaji tuliyependana. Tuliishi pamoja miaka kumi; nikamzalia watoto watatu. Watu wazima sasa hivi. Nina wajukuu saba na kitukuu kimoja.”
Namuuliza kama baba watoto yuko hai.
“Mungu keshamchukua. Alikuwa freshi sana. Ila alifanya kosa moja. Hali kabla ya kunywa; na akinywa hafanyi kazi. Mi bado nachapa kazi za kujitolea hospitali za wazee ingawa nimeshastahafu. Mwezi ujao natimiza miaka 70. “
Anacheka.
Kwanini hakurudi kwao visiwani, Jamaika?
“Mi si Mjamaika. Unaona mlivyo mabwege? Mkimwona mtu mweusi mnasema anatoka Nigeria au Jamaika. Kwetu ni Montserrat. Unapajua?”
Ni kule mlima ulipotoa volcano mwaka 1997?
“Huko huko. Nilitaka nirudi Montserrat lakini kwa kuwa mambo ya volcano yameanza tena; nitafia hapa hapa Uingereza.”
Anacheka.
Tumefika kwake.
Namuuliza vipi akakatiwa jina la Malkia Maria?
“Yule binti ananjua...Namfahamu toka akizaliwa. Wazee wake matajiri lakini babake alikuwa fisi. Alikuwa akiwapiga wote, mama na watoto. Watoto wote wa yule mzee wameharibika. Yeye mwenyewe kahamia Hispania. Aliwaachia nyumba na utajiri lakini kutokana na hali ngumu aliyowafanya wakiwa wadogo akili zao hazikuwa nzuri; wakapoteza hela katika dawa za kulevya.”
Kesho yake ninapompitia Vivian namwangalia kwa macho mengine.
Nchi hii tajiri lakini ina kila aina ya mambo.
Kwetu Afrika umaskini hutokana na wachache kuwa na mali na kutowapa wengi. Hutokana na viongozi wasiojali watu wao na kujilimbikizia mali kama ilivyokuwa Misri. Mbabe yule katawala toka mwaka 1981 bila kukubali uchaguzi; akiwafunga waliodai haki yao, akiwapendelea wenzake na ndugu zake; akijaza mabilioni ya pesa nje ya Misri aliyodai anaipenda. Hicho ndicho kinachotudidimiza Afrika; kujenga umaskini ndani ya bara hili tajiri kushinda yote duniani.
Sasa linganisha na ufukura ulioko nchi zilizoendelea.
Omba omba na maskini wapo.
Mna hohehahe lakini si wote wanatoka familia maskini za matabaka ya chini. Ufukara, huzuni au ukiwa wao husababishwa na mambo ya kila aina.
Vivian alizaliwa mwaka 1986. Babake alikuwa mfanya biashara mkubwa. Kutokana na hali yake ile alipenda sana kazi kuliko watoto. Kwa kuwa akiwa nao watoto anakuwa amechoka huonyesha mapenzi yake kwa kuwapa zawadi na pesa. Na siku moja moja mkewe akimkorofisha anamnyuka. Watoto wakilia anawatandika vile vile. Hatimaye mkewe akatoroka na mwanaume mwingine. Akamwachia watoto wale; wawili wa kike, mmoja mwanaume. Baba mtu alivyokuwa punguani akawa anawaharibu, analala nao. Ndivyo alikoanzia hadi leo binti kageuka omba omba, kaharibikiwa.

-London, Jumatatu, 14 Februari, 2011
-Ilitoka Mwananchi, 20 Feb, 2010

Monday, 7 February 2011

HAJA NDOGO NJE KWA WANAWAKE SI JAMBO RAHISI...

Tupo sebuleni kwa jirani yangu mmoja mwanamke. Katualika majirani kusherehekea siku ya kuzaliwa miaka themanini. Themanini nakwambia! Wanawe wawili wamewasili na wajukuu na vitukuu toka Australia na Afrika Kusini kushangilia siku hii maalum ya ajuza mcheshi, roho safi; kibibi anayependwa na kila mtu hapa mtaani ninapoishi London. Nyumba imetota baraka. Harufu mbalimbali za makulaji zinazitesa pua. Vyakula vimetandazwa mezani. Viazi Ulaya vya kuchemsha na kuoka vinavyotengeneza msosi maarufu uliovum buliwa na hawa hawa Waingereza unaojulikana kama Chips. Mboga mbichi safi za saladi, nyanya, matango, vitunguu, jibini (chizi), mikate ya kila sampuli, samaki na kuku wa kukaanga. Kawaida karamu za Majuu hutenganisha walaji wa nyama na wasiokula nyama (Vegetarians).

Sunday, 9 January 2011

KUJIENDELEZA, MAZOEZI NA KUINUA VYUMA -Sehemu ya Mwisho

Makala kadhaa zilizopita zimesisitiza sisi wananchi wenyewe kujiendeleza. Lengo la insha hizi ni kukumbusha wewe mwananchi kwamba huwezi kusonga mbele bila elimu na maarifa sahihi; kwamba maendeleo yanawezekana.
Jamii ya Marekani imejenga utamaduni huu uitwao Self Help. Ni utamaduni uliozalisha biashara ya vitabu, video, magazeti na vipindi mbalimbali vya runinga vinavyosisitiza mwananchi kujituma badala ya kutegemea uchawi, dini au imani nyingine peke yake. Lengo ni kuweka nguvu za kimaendeleo mikononi mwa mwanadamu. Kelele inayopigwa ndani ya utamaduni wa Kimarekani ni kuwa lolote linawezekana kwa anayejitahidi.

Sunday, 2 January 2011

MAAZIMIO YAKO 2011 YAWE KUJIENDELEZA KIFIKRA...

Kabla ya kuendelea na mada ya mazoezi tuliyoiongelea Jumapili iliyopita tuutazame mwaka mpya 2011, kijasiri. Msomaji huenda hufurahishwi na hali ya uchumi, wanasiasa wanaotuongopea na maisha yanayoendelea kuwa  magumu.
Hisia hii imeenea ulimwenguni. Imekithiri kiasi ambacho kuna fikra mwisho wa dunia unakuja. Wapo wanaoeneza falsafa kwamba mtabiri wa zamani Nicodemus aliambiwa na Yesu Kristo kuwa dunia itakwisha 2012. Mfano mzuri ni blogu la “2012 Doomsday Prophecies” (Tabiri za Siku ya Kiama 2012) linalonukuu Biblia (Yohanna Sura ya 3:8) na hali ya mafuriko, matufani na matetemeko makubwa miaka hii (Haiti, 2010) kama ishara ya angamio hilo.
<!--more-->
 Bila shaka msomaji umesikia namna msimu wa barafu ulivyokuwa mkali Ulaya na Marekani. Usafiri umeathiriwa, watu 60 walifariki mwezi Desemba nchini Ujerumani, Urusi, Ubeljiji na Poland. Viwanja vya ndege vimedhurika na safari kuvunjwa.
Blogu la “Doomsday” linapiga makofi kusifia ukweli wa tabiri zake Nicodemus. “Doomsday” linatukuza kalenda ya Maya inayosisitiza mwisho wa ulimwengu na mwanzo mpya...
Barani Afrika, leo, imani kuwa uhai umelaaniwa zimeshika hatamu. Kutokana na maafa ya vita, magonjwa ya UKIMWI na malaria, Waafrika wengi waliodhalilishwa na viongozi waongo wanaowaibia na kuwadanganya kila siku wamekimbilia dini. Imani zetu za jadi ambapo mababu na mabibi zetu walitambikiwa na kuaminiwa  zimetupwa shimoni. Badala yake wengi tuko tayari kupigana hadi kufa kutetea dini zilizoletwa na wageni miaka michache tu iliyopita. Dini hizi zinazotukuza upendo, amani na Mungu kuwa suluhisho zimekuwa ndiyo ahueni ya mawazo na hisia. Kimsingi wanadamu dunia nzima tunaupokea mwaka 2011 kwa utata.
Je, ni kweli mwisho wa dunia utakuwa 2012?
Mwezi ujao natimiza miaka 56. Toka nikiwa mtoto nimezisikia hadithi hizi za mwisho wa dunia. Mwaka 1962 nikiwa darasa la kwanza hofu iliyoenea ilikuwa bomu la Atomiki na vita vikuu vya tatu vitakavyotokea kutokana na uhasama baina ya Wamarekani na Warusi. Uhasama uliota kichuguu wakati Rais Fidel Castro wa Cuba na makamu wake Che Guevara walipoamua kumwambia Mmarekani afilie mbali, asiendelee kuonea mataifa na watu maskini. Mgogoro wa Cuba na Marekani, 1962, uliitisha dunia nzima. Na haukuwa wa kwanza miaka ya Sitini. Uliendelea Vietnam, Kongo na hata Zanzibar. Kila mahali wanadamu walipojaribu kudai haki zao toka ukoloni na hali ngumu kiuchumi walitishwa na tembo wawili yaani Urusi na Marekani.
 Kipindi chote nilichosoma shule ya msingi hadi naingia sekondari 1969 kilikuwa cha hofu ya bomu la Atomiki; kwamba dunia italipuka dakika yeyote. Tukiwa watoto habari hizi zilichanganya migogoro ya kivita Vietnam, mauaji ya viongozi mashuhuri  Rais John Kennedy wa Marekani (1963), Malcolm X (1964), Martin Luther King (1968) na Waziri Tom Mboya wa Kenya aliyepigwa risasi mjini Nairobi, 1969.
Miaka ya Sabini ilizidi kuchubua.
 Kila mahali wanadamu walidai haki zao, wakipingana na tawala zilizowatesa. Hapa Bongo migomo ilitokea viwandani, mashuleni na moja ya mambo makubwa  ni kuuawa kwa  Rais wa kwanza Zanzibar, Abeid Amani Karume, mwaka 1972. Bara zima la Afrika lilichachamaa  na wapigania Uhuru, Angola, Msumbiji, Namibia, Zimbabwe, nk. Nchi zilipinduliwa  na lililotuathiri zaidi Wanabongo ilikuwa Jemadari Idi Amin Dada aliyemtoa Rais Milton Obote madarakani  Uganda, mwaka 1971.
 Kilichonguruma zaidi ni Wapalestina. Wanaharakati waliteka nyara ndege wakidai kutambuliwa; huku nyuma nchi tajiri za Kiarabu zilizotoa petroli zikipandisha bei mafuta hayo kuwakamua matajiri wa Ulaya na Marekani walioisaidia Israeli dhidi ya Wapalestina. Hapa ndipo mgogoro uliopo leo Mashariki ya Kati na Afghanistani ulipoanzia. Ndege zilitekwa nyara na tatizo la Wapalestina likajulikana. Wakati haya yakiendelea  hali ya uchumi iliharibika kiasi ambacho nchi tajiri zilipunguza kabisa bei za mazao toka nchi changa. Uchumi mgumu tulionao leo ulikuwa pia taswira ya miaka ya Sabini. Kiama kilizungumziwa. Fasihi na sanaa vilijitahidi kuliwaza. Mwanareggae Bob Marley, toka Jamaika, aliimba kuhimiza mapenzi, amani na harakati.
Miaka ya Themanini iliangukiwa na UKIMWI. Mwanzoni UKIMWI ulisemekana tu  tatizo la wasenge. Ila mwaka 1987 UKIMWI ulienea hata wasiokuwa firauni. Afrika Mashariki UKIMWI ulikatiwa jina la SLIM kutokana na jinsi ulivyokondesha walioupata. Miaka ya Themanini na Tisini uliwapa Waafrika imani kuwa bara letu limelaaniwa. Laana iliraruka  mwaka 1994 kutokana na mauaji ya Watusi na Wahutu, laki nane, Rwanda.
Kiulimwengu miaka ya Tisini ilikuwa ya mauaji ya jumla jumla. Aprili 1995 mji wa Oklahoma, Marekani, ulistuliwa na gaidi Timothy McVeigh, aliyejeruhi 680, akaua   168, (kati yao watoto 19) na kuharibu majengo 324 kwa mabomu. Ni kipindi hiki kila mtu alipoongelea mwisho wa dunia yaani 1999 kuangukia, 2000. Mwanamuziki  wa Kimarekani, Prince alitunga wimbo uitwao 1999.
 Ugaidi na mabomu ya Waarabu walioudhiwa na siasa za Magharibi kuhusiana na Wapalestina wakiongozwa na Al Kaida ya Osama Bin Laden yalisambaa kuanzia Dar es Salaam (1998) hadi New York, Septemba 2001.
Kifupi hakuna kipindi chochote nilichoishi ambapo hapakuwepo  fikra kwamba mwisho unakuja. Ukishunguza historia yetu wanadamu kila kipindi  kimekuwa na vita au machafuko ya mazingira.
Msomaji zingatia kwamba masha yetu ni mseto wa mabadiliko, mvutano wa maumbile, mabaya na mazuri, moto na baridi, jike na dume, matajiri na maskini, wenye uwezo na wasio uwezo.
Je, utamuduje?
Mwaka 2008 nilimhoji mwanasaikolojia wa Kiingereza, Dk. John Conolly, pia mganga wa wenda wazimu. Alisema wagonjwa wa vichaa wanaongezeka duniani kutokana na baadhi yetu kushindwa kuyaelewa maisha ili kuyamudu. Alishauri kila mtu kujiuliza maswali akiamka au akienda kulala.
Unapoamka jiulize je, leo nitafanya jambo gani kujiendeleza kitaaluma?  Je, nitafurahishaje nafsi yangu? Na kama sina raha nitachukua hatua gani kukabili na kutawala mazingira na maisha yangu badala  ya kuyahofia?
Je Watanzania wangapi wanaazimia kununua kitabu mwaka huu kujisomea? Idara ya Elimu ya Umoja wa Mataifa mwaka jana ilikiri kwamba watoto 72 milioni duniani hawasomi;  na kwamba elimu ni tatizo mosi la jamii maskini ulimwenguni.
 Fidel Castro wa Cuba anasema katika kitabu cha maisha yake kuwa tumeumbwa kuuendeleza ulimwengu wetu. Tuko hapa tuwazae wanadamu wengine watakaochangia uhai.  Hivyo basi, mwaka 2011 uwe wako kujiendeleza, ndugu msomaji.

 -London, Jumanne, 28 Desemba,  2010.


Ilichapishwa gazeti la Mwananchi, Jumapili, Januari 2, 2011.


http://www.mwananchi.co.tz/mwananchi-jumapili/38-johari/7961-maazimio-yako-mwaka-2011-yawe-ya-kujiendeleza-kifikra