Niko hoteli kubwa la The Russet, katikati ya maskani ya wafanyakazi wa kawaida, kaskazini ya London. Nimealikwa kutumbuiza ngoma za Kiafrika. Mauzo ya sherehe hizo yatasaidia kijiji kimoja Tanzania. Watayarishaji ni shirika la urafiki baina ya Uingereza na Tanzania, BTS yaani British Tanzania Society. Janet Chapman na mwenzake Jonathan Pace, ni wale wazungu wachache wanaofikiria mazuri tu kuhusu Waafrika, hususan Watanzania.
Watu wa
makamo.
Miaka
30 iliyopita Janet alifanya kazi ya
ualimu Sudan, vijijini; akichanganyika
na wakulima na wafugaji maskini. Kati ya jambo ambalo hakulipenda ni mila ya
kuwatahiri wasichana wadogo au kwa Kiswahili cha kileo, ukeketaji. Janet anasema kwa kuwa mwenyewe alikuwa na
mabinti wadogo wawili- ambao leo wameshakuwa watu wazima- yalimgusa sana. Baadaye
aligundua adha hii imeenea nchi nyingi bara Afrika, Mashariki ya Kati na Asia.
Takwimu za shirika la Afya duniani (WHO) zinakadiria
wasichana na wanawake milioni 91 na nusu barani wamekeketwa. Kati ya hawa
milioni 12 na robo wana umri mdogo wa miaka 10 hadi 14. Tovuti la habari za ukeketaji (FGM) linadai
nchi 26 za Kiafrika, ikiwemo Tanzania zinabeba bendera ya ukeketaji. WHO inafahamisha
kati ya wanaotetea adha hii ni mama wazazi waliokeketwa na baadhi ya wanaume.

