Showing posts with label The Russet London. Show all posts
Showing posts with label The Russet London. Show all posts

Monday, 16 June 2014

USIKU KUCHANGIA JENGO LA WASICHANA WANAOKWEPA UKEKETAJI TANZANIA


Niko hoteli kubwa la The Russet, katikati ya maskani ya wafanyakazi wa kawaida, kaskazini ya  London. Nimealikwa kutumbuiza ngoma za Kiafrika. Mauzo ya sherehe hizo yatasaidia kijiji kimoja Tanzania. Watayarishaji ni shirika la urafiki baina ya Uingereza na Tanzania, BTS yaani British Tanzania Society. Janet Chapman na mwenzake Jonathan Pace, ni wale wazungu wachache wanaofikiria mazuri tu kuhusu Waafrika, hususan Watanzania.
  Watu wa makamo.
Miaka 30 iliyopita  Janet alifanya kazi ya ualimu Sudan,  vijijini; akichanganyika na wakulima na wafugaji maskini. Kati ya jambo ambalo hakulipenda ni mila ya kuwatahiri wasichana wadogo au kwa Kiswahili cha kileo, ukeketaji.  Janet anasema kwa kuwa mwenyewe alikuwa na mabinti wadogo wawili- ambao leo wameshakuwa watu wazima- yalimgusa sana. Baadaye aligundua adha hii imeenea nchi nyingi   bara Afrika, Mashariki ya Kati na Asia.

 Takwimu za shirika la Afya duniani (WHO) zinakadiria wasichana na wanawake milioni 91 na nusu barani wamekeketwa. Kati ya hawa milioni 12 na robo wana umri mdogo wa miaka 10 hadi 14.  Tovuti la habari za ukeketaji (FGM) linadai nchi 26 za Kiafrika, ikiwemo Tanzania zinabeba bendera ya ukeketaji. WHO inafahamisha kati ya wanaotetea adha hii ni mama wazazi waliokeketwa na  baadhi ya wanaume.