Showing posts with label Shenge. Show all posts
Showing posts with label Shenge. Show all posts

Thursday, 4 April 2013

USONGO WANGU NA KISWANGLISHI : WATANZANIA HATUJAKOMAA KILUGHA-2


Kusoma na kutukuza fasihi  ya Kiswahili Fasaha kupitia vitabu na sinema  ndiyo njia pekee itakayoendeleza na kuimarisha lugha yetu...

Wiki jana tuliangalia namna ambavyo Kiswahili kimekua, kikazoa na kuburuta misamiati  ya lugha za Kiarabu, Kiingereza, Kiajemi, Kireno, Kihindi nk. Hapo hapo kanuni zake za kisarufi (“grammar”) ni za Kibantu. Ina maana Kiswahili ni lugha ya Kiafrika, inayojitosheleza.
Kukua kwa “Kiswanglish” si jambo baya. Tatizo hili si geni barani Afrika.Wala si geni ndani ya baadhi lugha mbalimbali ulimwenguni. Waspanyola wakazi wa Marekani wameunda “Spanglish”- lugha ya mitaani inayotumiwa  na walowezi waliozaliwa kule walio baina ya utamaduni wa Kimarekani na Kilatina. Tofauti ni kwamba Walatina huwalea wanao kufuata mila zao. Si kama Waafrika wengi wanaokulia Majuu- hawasisitizi wanao huku Uzunguni kuzijua mila na lugha zao. Wanaona nishai na aibu... kwamba lazima wafanane na wenyeji.
Amina Waziri ...mjukuu wa Shaaban Robert ambaye ni mmoja wa waalimu wakubwa wa Kiswahili Ughaibuni akiongea nami mwaka 2008 kuhusu haja ya kutukuza kumbukumbu ya babu yake na kuendeleza lugha hii muhimu. Picha na F Macha

Wiki jana tuliangalia namna Kenya ilivyoanza lugha ya Shenge, miaka 20 iliyopita. Lugha hii ilichanua kutokana na baadhi ya Wakenya-hasa mjini Nairobi- ambao ni wazungumzaji wazuri wa Kiingereza kuwa dhaifu katika msamiati wa Kiswahili na kuamua kuchanganya changanya. Lakini haina maana walikua duni lugha ya Kiingereza. Sisi tunaingiza Kiingereza katika Kiswahili- lakini tunasutwa (hasa na majirani wetu wa Kenya na Uganda) tulivyo wabovu kwa Kiingereza. Kabla ya kuendelea – hebu tuangalie nchi nyingine ya Kiafrika zenye mtindo wa kupikicha pikicha lugha kama Kenya.

Sunday, 24 March 2013

USONGO WANGU NA KISWANGLISHI : WATANZANIA HATUJAKOMAA KILUGHA- 1


Karibuni, Baraza la Waganga Uingereza lilipitisha sera ya kutomruhusu daktari wa kigeni kufanya kazi bila kufuzu mtihani wa Kiingereza fasaha. Ina maana ili kutibu wagonjwa lazima uimanye lugha ya wenyeji vizuri. Wenyeji wanathamini sana lugha yao mama- bila kuichanganya nganya na kuibandika  bandika viraka.
Mwandishi maarufu wa Kiswahili fasaha, Adam Shafi akiwa Uingereza mwaka 2007. 
Picha na F. Macha

Msemaji wa Baraza hilo alipohojiwa na runinga ya “Sky” alijitoa mwenyewe kama mfano:
“Nilisoma Kifaransa nikiwa sekondari. Ninaweza kuongea Kifaransa cha kuombea maji. Ila nilipofanya kazi kwao  kama mganga nlikua na matatizo maana sikuyajua maneno au misemo ya taaluma ya uganga ipasavyo. Ikabidi niende kozi. Ni hatari sana kutibu watu kama unaboronga lugha.”
Akiwa na maana kujua lugha juu juu au sawasawa ni mambo mawili tofauti. Wenzetu waliondelea wanathamini sana kufahamu lugha sawasawa badala ya kubabaisha.
Nimetathmini sera hiyo ya Waingereza ili kuongelea suala la Ki-Swanglish ambacho kinaendelea kuzaa chawa Tanzania. Miezi michache iliyopita nilikua kwenye kikao na kundi la Wabongo wenzangu hapa Ulaya, mzalendo mmoja akauliza: “ Bwana Macha hapendi sana kuchanganya changanya maneno ya Kiingereza na Kiswahili.”
Kitabu kipya cha Adam Shafi- kinachoendeleza Kiswahili Fasaha. Picha toka Blog la KiSwahili Afrika Mashariki