Showing posts with label Wanahabari Tanzania. Show all posts
Showing posts with label Wanahabari Tanzania. Show all posts

Thursday, 13 February 2014

UBORESHAJI LUGHA NCHINI WATEGEMEA SANA WANAHABARI NA UJUZI WA FASIHI -1




Mzee Adam Shafi, mwandishi nguli aliyeanza shughuli zake kama mwanahabari zamani. Leo lazima kumsoma. Umahiri wake wa lugha hausemeki. Picha na F Macha, 2007.


Wiki iliyopita kulikuwa na mdahalo na majadiliano moto bungeni. Lugha ipi itumike kufundisha watoto wetu mashuleni? Tatizo hili si ngeni kwa nchi zinazotumia zaidi ya lugha moja kimawasiliano. Wakati ninaishi Canada miaka iliyopita niliepuka matatizo kwa vile kitongoji nilichoshukia kiliongea zaidi Kifaransa. Nilikuwa nimekwenda kusoma  mwaka mmoja. Kawaida Mtanzania unapofika  nchi isiyozungumza Kiingereza- hubidi utumie wastani wa mwaka mmoja kujifunza lugha. Haya yamewasibu wanafunzi waliokwenda Urusi, Ujerumani, China, Cuba nk.
Mwandishi nikifanya shughuli ya kutengeneza bustani, Canada, mwaka 1995...picha na S Vanessa.

Canada inazo lugha mbili : Kiingereza na Kifaransa.  Bahati  yangu wakati nikifanya kazi magazeti ya Uhuru na Mzalendo,  nilijifunza Kifaransa na ingawa ujuzi wa lugha hiyo si mzuri kama Kiingereza, ilinisadia sana masomoni.