Sunday 17 March 2019

MARADHI YA FIGO NA FAIDA ZA KUFUNGA KULA- 4



Maradhi ya figo yamezidi sana kwa watu weusi, seuze Watanzania.
 Majuma mawili yaliyopita tulimpoteza Mtanzania maarufu sana kwa ugonjwa huu. Ni muhimu kujadili kwanini figo linaendelea kuwa tatizo kubwa kwetu.
Makala tatu zilizopita zimeongelea ulaji wa Saladi, mazoezi na kufunga kama njia za kujali figo, ini, moyo, ubongo,nk. Tumeambiwa  matumizi HOLELA ya dawa za kuzuia maumivu  changia tatizo au pia fadhaa (“stress”) dhalilisha figo.
Wiki iliyopita tulikumbushana kuwa kufunga  si tu Ramadhani au Uislamu.Tulitazama faida zake ikiwepo kupunguza unene, maradhi, kuupumzisha mwili na uwezekano wa kuwa na maisha marefu.
Tulitazama aina ya kwanza ya ufungaji, yaani kunywa  maji ( kidogo kidogo kwa wastani wa saa 36-72).


Ni vizuri maji hayo yakichemshwa,  kama chai.  Nilijifunza dhana hii kwa Wachina wanaoshauri ikiwa ndani ya mwili ni joto (damu) vyema kujimiminia vile vile kitu cha moto.  Maji wakati wa kufunga husafisha figo.
 Mfungo wa pili ni kutokula  chochote  (“dry fasting.”)
 Faida na matokeo huwa  haraka zaidi kuliko kufunga kwa maji. Kila aina ya kirusi, maradhi au tatizo hutoweka upesi. Zingatia unapofunga, baada ya saaa 21 virusi adui mwilini hukosa chakula na kuanza kusambaratika. Ukinywa maji huchukua muda zaidi. Tuseme baada ya saa 36.
Mfungo wa tatu ni kunywa juisi (ya  matunda au mboga) kidogo kidogo kwa muda takikana.
Wa mwisho ndiyo unaokua haraka sana Ughaibuni.  Unaitwa  “Intermittent fasting.” Pendwa sana na  wanaodhamiria kupunguza unene au uzito.  Mfano unakula chakula  kidogo tu asubuhi. Jioni huli. Kesho unakula jioni.  Unafuata kanuni hii kwa siku tatu, kisha unaanza  tena kula kawaida (mara tatu kwa siku)  hivyo hivyo kwa  majuma kadhaa. Ufungaji huu ni wa kudumu zaidi na unapozoeleka huwa desturi ya mtu.
Mtindo wowote utakaoamua  ni mzuri kwa afya yako.
La kuzingatia ni namna unavyofungua. Kula milo mizito au haraka haraka wakati wa kufungua si vizuri asilani. Unapofungua anza taratibu, ikiwezekana kwa matunda laini kama mapapai, matikitiki maji. Au kama hukunywa maji, anzia na maji moto kwa saa kadhaa.
Baadaye ndiyo vyakula vyepesi kama uji. Uji wenyewe usiwe na sukari na chumvi bali asali.  Baadaye ndiyo mlo mzito.
Si vyema hata kidogo kufungua kwa vyakula vizito kama nyama au mayai. Ukweli ikiwezekana usile nyama hadi siku ya pili au ya tatu.
Mwisho tukumbushane kuwa bado wapo wengi wenye fikra finyu kuhusu afya na kufunga.  Huamini eti maradhi  au kifo ni “kudra ya Mungu.” Dhana hii inaturudisha sana Waaafrika nyuma. Tunaweka kila adha mikononi mwa Mungu huku wenzetu wanasonga mbele. Wapo wanaosema kufunga ni kuendekeza njaa.  Hawaelewi kuwa faida ya kufunga ni fikra pevu, mwili safi, ubongo imara na maisha marefu.   Askari wa Kizungu waliokamatwa mateka na Wajapani wakati wa vita Vikuu vya Pili wakanyimwa kula waliishi zaidi ya miaka 90 hatimaye.
Ndiyo maana wanyama wakiugua, hawali. Au kama ni paka au mbwa hula majani. Tujiulize kwanini.
Dini ZOTE duniani zina kipengele cha kufunga. Wanaofuata kanuni  kwa dhati huwa Waislamu na Wayahudi. Wengine tumesahau au hatutunuku masharti ya imani zetu mahsusi.
  


No comments:

Post a Comment